Mechi za pili za raundi ya mtoano kwa timu 16 za Ligi ya Ulaya (Uefa Champions League) zinatarajiwa kuanza tena kupigwa usiku wa leo Jumanne Machi 7 kwa mechi mbili, ambapo huko katika dimba la Emirates Jijini London, Uingereza wenyeji Arsenal watawakaribisha Bayern Munich huku wakiwa na kumbukumbu ya kipigo cha 5-1 walichoshushiwa katika Mechi ya kwanza iliyochezwa huko Ujerumani.
Ili kufuzu kuingia hatua ya robo fainali ya michuano hiyo, timu ya Arsenal inapaswa kufanya kitu ambacho hakijawahi kufanyika kwa urahisi kwa kushinda 4-0 au kwa idadi nyingine ya Mabao ilimradi tofauti ya Magoli iwe 4-0 dhidi ya wageni wao hao.
Mechi ya pili ya leo itachezwa huko Naples, Italy wakati wenyeji Napoli itawakaribisha kwa mchezo wa marudiano Mabingwa watetezi wa michuano hiyo, Real Madrid huku wakihitaji ushindi wa bao 2-0 kwa kuwa mchezo wa awali walichapwa 3-1 huko Santiago Bernabeu Jijini Madrid, Hispania kwenye Mechi ya Kwanza.
Napoli pia wanaweza kufuzu ikiwa watashinda kwa idadi nyingine ya Mabao ilimradi tofauti ya Magoli iwe 2-0.
Kesho, Jumatano Machi 8 zipo Mechi nyingine 2 ambapo Barcelona itakipiga na Paris Saint Germain, huku PSG wakiwa mbele kwa mabao 4-0 na mechi ya pili ni kati ya Borussia Dortmund na Benfica huku Benfica wakiongoza 1-0.
Mechi za pili za raundi ya mtoano kwa timu 16 za Ligi ya Ulaya zitakamilika, Machi 14 na 15, kwa Mechi nyingine 4 ili kutoa Washindi watakaocheza robo fainali.