Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.
Hatimaye Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini (TFF) limeweka wazi kuwa uwanja Jamhuri mjini Ddodma ndio utakaotumika kwa ajili ya fainali ya mchezo wa Fainali za kuwania Kombe la Shirikisho la Azam (Azam Sports Federation Cup HD - ASFC) mwaka huu.
Hayo yamesemwa leo na Rais wa TFF Jamal Malinzi wakati akifungua kozi ya uamuzi na ukocha inayoendeshwa na Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Ubungo (UFA) na kuweka wazi kuwa fainali ya Kombe la FA itafanyika katika uwanja wa Jamhuri Mkoani Dodoma.
Fainali hiyo kati ya Simba SC ya Dar es Salaam na Mbao FC ya Mwanza, itafanyika Mei 28, mwaka huu huku kila timu ikiwa ni wageni kwenye uwanja huo ambapo makao makuu ya nchi.
Kwa mujibu wa Kanuni ya 5 ya michuano ya ASFC kuhusu Uwanja wa mashindano inasema: “Uwanja wa mashindano ya Kombe la Shirikisho la Azam Sports HD utakuwa ni uwanja wenye hadhi inayokubalika na TFF.”
Hilo limekuja baada ya jana Rais wa TFF kunukuliwa katika mtandao wake wa kijamii wa Twitter akisema kuwa, kutachezwa kwa droo ya kutafuta wapi fainali ya Shirikisho itachezwa huku wadau mbalimbali wakionekana kupinga suala hilo na kusema haiwezekani na haijawahi kutokea.
Simba walifanikiwa kutinga hatua ya fainali baada ya kutoka na ushindi wa goli 1-0 dhidi ya Azam mchezo ukiofanyika April 29 katika dimba la uwanja wa Taifa, na Mbao kuivua ubingwa Yanga kwa kuifunga goli 1-0 mechi iliyopigwa April 30 dimba la CCM Kirumba Mwanza.