Na John Nditi, Morogoro
SERIKALI ya mkoa wa Morogoro imetoa Sh milioni kumi kwa ajili ya kununua unga na maharage kwa ajili ya waathirika 8,800 wa mafuriko yalitotokea katika vijiji kadhaa vya halmashauri ya wilaya ya Morogoro.
Mbali na mkoa pia halmashauri ya wilaya imetoa Sh milioni tatu kwa ajili kununua mahitaji muhimu kwa waathirika wa mafuriko hayo kwa wananchi wa vijiji vya kata tatu zilizopo katika halmashauri hiyo.
Hatua hiyo imetokana na Mkuu wa mkoa huo, Dk Kebwe Steven Kebwe na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa kutembelea eneo la mafuriko Aprili 26, mwaka huu kwa kutumia helikopta ya Polisi na kujionea hali halisi , ambapo pia aliongea na waathirika wa kijiji cha Bwila juu , Kubulumo na Kiganila.
Mkuu wa mkoa , Dk Kebwe alisema na kiasi hicho cha fedha , zimewezesha kununua tani sita za unga wa sembe na tani mbili za maharage , mafuta ya kupiki na chumvi na kupekewa kwa waathirika kwa kutumia magari makubwa mawili ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Mkuu wa mkoa kabla ya kukabidhi msaada huo wa awali kwa mkuu wa wilaya ya Morogoro, Muhingo Rweyemamu, alisema licha ya wananchi hao kupatwa na mafuriko ,aliwataka eneo wanaloishi kuhama kwa kuwa tayari walilipwa fidia kupisha ujenzi wa bwawa la Kidunda.
“ Tunatoa mdaada huu kutokana na hali ya kibinadamu ingawa tayari walitakiwa kuhama maeneo yao kwa ajili ya kupisha ujenzi wa bwawa la Kidunda baaada ya serikali kupita fidia ...lakini wamendelea kubakia na sasa wamekubwa na mafuriko haya” alisema Mkuu wa Mkoa.
“ Hiki chakula kinatolewa kwa awamu ya mwisho , hakitatolewa kingine , na nina agiza Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri , Mwenyekiti wa halmashauri pamoja na Mkuu wa Polisi wilaya , watu hawa waondoke maeneo hayo kwa kuwa tayari wamepimiwa viwanja na kulipwa fidia zao” alisisitiza Dk Kebwe.
Alisema ,kama zilipitika siasa wakati wa uchanguzi mkuu uliopita na kuwafanya waendelee kubakia maeneo hayo kwa sasa imekwisha na hawana budi kuyahama maeneo hayo wakati taratibu za kumaliziwa malipo y ao za ziada zilifanyiwa kazi na Serikali.
Naye Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Yona Maki , alisema licha ya kupatiwa msaada wa awali, pia mahitaji muhimu yanahitajika kwa haraka lambayo ni mahema 20 kwa ajili ya makazi kwa waathirika 200 waliotoka kijiji cha Bwila chini na kuhamia eneo la muinuko katika kijiji cha Msonge.
Maki pia alitaja mahitaji mengine ni pamoja na kupatiwa boti mbili za kuvusha waathirika na kuwapekelea mahitaji yao ng’ambo ya pili yam to sambamba na mbegu za mahindi tani 26 na mtama tani 1.4 ikiwemo muhongo na viazi vitamu na dawa za binadamu.
“ Waathirika wanaohitaji msaada hadi sasa ni 8,795 kutoka vijiji vitano vya Kata ya Serembara, vijiji viwili kata ya Mvuha , kijiji kimoja kata ya Tununguo na kijiji kingine kimoja kutoka kata ya Mkulazi” alisema Maki.
Kwa upande wake , Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo, Kibena Kingo, alisema kuwa pamoja na wananchi walioathiriwa na mafuriko kulipwa fidia inayikadiriwa Sh bilioni saba na kupewa viwanja kwa ajili ya kuhamia kupisha ujenzi wa bwawa la Kidunda.
Pamoja na hayo alisema ,wananchi wa vijiji Kibulumo, Bwila chini , Bwila juu na Vidunda waliolipwa fidia walishindwa kuyahama makazi yao baada ya kuwasilisha madai mapya kuwa wamepunjwa fidia zao
Mwenyekiti wa halmashauri hiyo pamoja na Mkurugenzi mtendaji wake kwa nyakati tofauti walisema wananchi waliotakiwa kuhama eneo hilo la bonde ili kupisha ujenzi wa bwawa la Kidunda walilipwa fidia jumla ya Sh bilioni saba na b ado kulipwa nyongeza ya fidia ya Sh bilioni nne.
Mkuu wa mkoa wa Morogoro, Dk Kebwe Steven Kebwe ( wapili kushoto) akikabidhi kiroba cha sembe kilo 50 ikiwa ni sehemu ya tani sita ya unga huo, kwa Mkuu wa wilaya ya Morogoro, Muhingo Rweyemamu ( watatu kulia) Aprili 28, mwaka huu baaada ya Ofisi ya Mkuu mkoa kutoa Sh milioni kumi ya kununua vyakula kwa ajili ya kutoa msaada kwa waathirika wa mafuriko katika vijiji kadhaa vya Halmashauri ya wilaya ya Morogoro. (Picha na John Nditi). Sehemu ya chakula cha msaada kilichotolewa na Ofisi ya Mkuu wa mkoa kusaidia waathirika wa mafuriko.