Na Bashir Yakub.
Wapo watumishi wa umma ambao wameachishwa kazi kwasababu mbalimbali na wanahisi kuwa pengine haki haikutendeka lakini hawajui la kufanya. Basi waelewe la kufanya lipo na ni rufaa.
Na wengine wanajua kuwa ni rufaa yumkini wasijue rufaa yenyewe inakatwa kwa utaratibu upi. Nitaeleza hapa, lakini kwanza tujue nani mtumishi wa umma anayeongelewa hapa.
1.NANI MTUMISHI WA UMMA.
Sheria namba 8 ya 2002, Sheria ya Utumishi wa Umma , iliyofanyiwa marekebisho na Sheria Namba 18 ya 2007 imemueleza mtumishi wa umma. Kifungu cha 3 kinasema kuwa mtumishi wa umma ni yule anayefanya kazi katika ofisi yoyote ya umma. Ili uelewe vizuri mtumishi wa umma anayeongelewa katika sheria hii na katika makala haya ni yule mfanyakazi/mwajiriwa wa serikali. Kwahiyo watumishi wa bunge, maafisa wa mahakama, na wafanyakazi wa taasisi/kampuni binafsi taratibu hizi za rufaa zinazoelezwa humu haziwahusu.
Tunaongelea watumishi wa serikali kuu, za mitaa, mashirika ya umma, idara na taasisi zote zilizopo chini ya serikali tukiondoa wale wa uteuzi japo nao wanaongozwa na sheria hii.
2. HAKI YA RUFAA.
Unapokuwa umesimamishwa kazi rufaa ni haki yako ewe mtumishi. Rufaa sio kuonesha ukorofi, sio kuwa mjuaji, sio kupingana na serikali, na sio kukosa utiifu. Rufaa ni haki kama zilivyo haki nyingine za mshahara, likizo, nk. Usiogope kukata rufaa kwani hata huyo aliyekusimamisha kazi naye akisimamishwa anakata rufaa.
Kifungu cha 25( 1 ) (b) cha Sheria ya utumishi wa umma ndicho kinachoeleza haki hii. Kadhalika kwenye barua yako ya kuachishwa kazi au siku ya kusimamishwa, yafaa na ni haki uelezwe haki hii ya rufaa.
KUSOMA ZAIDI sheriayakub.blogspot.com