*Waziri Mkuu amtaka amalize migogoro ya wakulima, wafugaji
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Eng. Evarist Ndikilo apige kambi katika kata ya Miono wilayani Bagamoyo na kuwasaka wafugaji wanaopiga wakulima.
Waziri Mkuu alitoa agizo hilo wakati akizungumza na wakazi wa kata hiyo ambao walisimamisha msafara wake wakati akienda kukagua miundombinu ya Hifadhi ya Taifa ya Saadani iliyoko wilayani Bagamoyo, mkoani Pwani.
Akitoa kero za eneo hilo, Diwani wa Kata ya Miono, Bw. Juma Mpwimbwi alisema kata hiyo inakabiliwa na tatizo la wakulima kupigwa na wafugaji na wakipelekwa kituo cha polisi hawachukuliwi hatua yoyote.
“Wafugaji wanatupiga lakini wenzetu hawachukuliwi hatua na hata ukienda kushtaki polisi, hawakai kwa sababu wanadai wao wana fedha,” alisema diwani huyo.
Pia alisema mbali ya kero sugu ya maji, waliahidiwa barabara ya lami tangu miaka saba iliyopita lakini hadi sasa hawana hata kipande kidogo tu cha barabara hiyo.
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa (pichani kulia) akiwa ameongozana na Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Eng. Evarist Ndikilo alipofanya ziara ya kikazi mkoani humo.