Raisi wa Uganda, Yoweri Kaguta Museven amelaani mauaji ya Msemaji wa jeshi la polisi nchini Uganda ambaye pia alikuwa ni Naibu Mkuu wa Jeshi hilo, Andrew Kaweesi na walinzi wake wawili ambao walishambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana katika eneo la Kulambiro, Kisaasi kaskazini mashariki mwa mji mkuu Kampala, Nchini Uganda jana.
Bado haijajulikana sababu hasa ya kutekelezwa mauaji hayo ingawa serikali imeagiza kufungwa kwa kamera za usalama katika miji mikubwa yote nchini humo wakati huu uchunguzi ukifanywa.
Katika kipindi cha miaka saba iliyopita takribani matukio ya mauaji 12 yametekelezwa na washambuliaji waliokuwa wakiendesha pikipiki maarufu kwa jina la boda boda ambao walitoroka eneo la tukio na kutopatikana licha ya jitihada za polisi kuendelea kufanyika kuwatafuta.
Kwa mujibu wa Luteni Jenerali, Henry Tumukunde, mara nyingi vitendo hivi hufanyika kwa umakini kujiamini na ujasiri huhakikisha wameua kabisa kabla ya wauaji kutokomea.