Serikali imewataka viongozi wa kisiasa pamoja na watendaji wa serikali kutotumia madaraka yao vibaya kuwanyanyasa na kuwasumbua wawekezaji wazawa waliowekeza ndani ya nchi.
Aidha viongozi hao wametakiwa kuwaheshimu na kuwajengea mazingira rafiki yatakayowawezesha kufanya biashara zao kwa amani ili kuweza kukuza uchumi wa taifa na kuongeza ajira kwa vijana. Kauli hiyo imetolewa jana na Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji Prof. Adolf Mkenda mkoani Simiyu, wakati wa sherehe za uzinduzi wa mwongozo wa uwekezaji wa mkoa huo pamoja na tovuti ya Mkoa.
Prof. Mkenda amewasihi viongozi wote wa serikali ngazi za mikoa na wilaya nchini kujivunia uwepo wa wajasiriamali na wafanyabiashara wakubwa ambao ni wazawa kwani wao ni chachu ya kuongeza kwa ajira za vijana.
Amesema kuwa si vyema wafanyabishara kutukanwa, kutolewa lugha zisizokuwa sahihi na kuonekana kama wana uadui na serikali, na badala yake watukuzwe ili kuweza kulipa kodi pamoja na kufuata sheria na taratibu za nchi.
“hawa wafanyabishara hasa wazawa na wajasiriamali tuwaone kama wenzetu, ndugu zetu na watu muhimu, kwani wameajiri vijana wetu, wanalipa kodi ili nchi ipate maendeleo, lakini wanatekeleza kauli mbiu ya Rais, Tanzania kuwa nchi ya viwanda, tuwathamni” alisema Prof.Mkenda. Katibu Mkuu huyo amezitaka halmashauri zote nchini kuhakikisha wanatenga maeneo kwa ajili ya wawekezaji wakubwa na wadogo kwa ajili ya kujenga viwanda.


