Mkuu wa mkoa wa Pwani, Mhandisi Evarist Ndikilo (wa nne kulia), akiwa katika picha ya pamoja na diwani wa Vigwaza Mohsin Bharwani (kulia kushoto kwake) pamoja na uongozi wa Lions club dar es salaam-Panorama baada ya kambi ya siku mbili ya huduma ya macho Vigwaza.
Na Mwamvua Mwinyi, Vigwaza
WAKAZI zaidi ya 20 wa kata ya Vigwaza, wilayani Bagamoyo,Pwani, wanatakiwa kufanyiwa upasuaji ili kutibu ugonjwa wa mtoto wa jicho. Akitoa taarifa katika kambi ya macho iliyofanyika shule ya msingi Vigwaza, mratibu wa taasisi isiyo ya kiserikali ya Lions Club Dar es salaam -PANORAMA, Prash Bhatti, alisema huduma ya macho waliyoitoa imegharimu kiasi cha mil. 30.
Alisema mbali ya kutoa huduma za macho, pia waliwahudumia wagonjwa wa kisukari, presha na kusaidia huduma za kijamii. Hata hivyo Bhatti alisema kambi hiyo ilikuwa ni ya siku mbili ambapo watu 2,000 walijitokeza kupima macho na kupata huduma ya miwani bure na zaidi ya 20 walikutwa na mtoto wa jicho.
"Shida kubwa ni ugonjwa wa mtoto wa jicho ambao kitaalamu tunaita cataract ugonjwa huu ndio unaoongoza kwa kuharibu jicho, dawa yake ni upasuaji"alisema.
Bhatti alielezea,watu hao waliogundulika na mtoto wa jicho watafanyiwa upasuaji na gharama zote zitatolewa na lions club.
Nae mkuu wa mkoa wa Pwani, mhandisi Evarist Ndikilo,alitoa wito kwa jamii kupima macho mara kwa mara ili tatizo libainike mapema na kutibiwa. Aliiasa jamiii kufanya matibabu ya mtoto wa jicho hospitali badala ya kukaa majumbani bila kujitibia.
Mhandisi Ndikilo, alisema tiba ya ugonjwa huo ni upasuaji na kuwa ulaji mzuri wa chakula na matunda hukinga macho dhidi ya magonjwa mbalimbali.
"Nampongeza diwani wa kata hii Mohsin Bharwani kwa kuona umuhimu wa kuwatumikia wananchi wake ikiwemo masuala ya kiafya"alisema mhandisi Ndikilo.
Diwani wa kata ya Vigwaza, Mohsin Bharwani aliishukuru taasisi hiyo kwa kujitolea kutoa huduma mbalimbali za afya na vitabu mashuleni.
Alifafanua kwamba watu wengi huwa hawapendi kuchunguza afya zao hivyo lions club imekuwa mkombozi kwao.
Bharwani, alishukuru pia kupokea msaada wa vitabu na madaftari kwa wanafunzi wa shule zilizopo Vigwaza.