Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali Bw.Mohamed Mtonga ametoa wito kwa wastaafu wanaolipwa Pensheni na Wizara ya Fedha na Mipango ambao ni wagonjwa na hawawezi kufika katika viwanja vya Karimjee na Mwalimu Nyerere(Sabasaba) kwa ajili ya uhakiki wa nyaraka zao kutoa namba za simu na majina yao ili waweze kuhakikiwa pale walipo kama ni Hospitali au nyumbani.
Bw.Mohamed Mtonga ametoa wito huo leo Jijini Dar es Salaam wakati akiongea na waandishi wa habari juu ya zoezi la uhakiki wa taarifa za wastaafu wanaolipwa pensheni na Wizara ya Fedha na Mipango linalofanyika katika Jiji la Dar es Salaam kuanzia leo tarehe 6-10 Machi.
“Kwa sasa ninavyozungumza zoezi hili liko kwenye hatua ya mwisho katika Mkoa wa Dar es Salaam,Zoezi hili lilianza Mkoa wa Pwani na tumelifanya nchi nzima na limefanyika kwa ufanisi mkubwa sana na wastaafu wengi wamejitokeza na kama mnavyoona zoezi limekuwa likiendelea kwa utaratibu mzuri sana”,Aliongeza Bw.Mtonga.
Mtonga amesema wastaafu hao wengi ni watumishi wa Serikali ambao walifanya kazi kabla ya mwaka 1999 ambapo walikuwa hawapo katika mifuko ya pensheni ndio ambao wanalipwa pensheni na Serikali wakiwemo watumishi wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Aidha amesema lengo kubwa la kuhakiki wastaafu hao ni kuboresha daftari la wastaafu ili kusaidia kujua ni kiasi gani cha wastaafu wapo katika kumbukumbu ya daftari la pensheni na kusisitiza wastafu ambao hawatajitokeza watafutwa katika daftari hilo.
Ukaguzi huu kwa mara ya mwisho ulifanyika mwaka 2014 na ukaanza tena mwezi Octoba mwaka 2016.
Uhakiki wa wastaafu wanaolipwa Pensheni na Wizara ya Fedha na Mipango wakiendelea na uhakiki katika viwanja vya Karimjee leo Jijini Dar es Salaam.Zoezi hili linafanyika kwa wiki nzima kuanzia tarehe 6-10 Machi kwa wastaafu walio Dar es Salaam.
Mkaguzi wa ndani kutoka Wizara ya Fedha na Mipango Bi.Mary Mauki akimpa maelekezo mstaafu wa Jeshi Bw.Rashid Hussein wakati wa uhakiki wa wastaafu wanaolipwa Pensheni na Wizara ya fedha na Mipango unaondelea katika Viwanja vya karimjee Jijini Dar es Salaam.
Muhasibu kutoka Wizara ya Fedha na Mipango Bw.Babu Kigule akizungumza na moja ya mstaafu juu ya utaratibu wa kuhakiki nyaraka za wanaolipwa pensheni na Wizara ya fedha na Mipango unaofanyika leo Jijini Dar es Salaam.
Wastaafu wanaolipwa pensheni na Wizara ya fedha na Mipango wakisubiri kuitwa kwa ajili ya kuhakiki nyaraka zao.Zoezi hili linafanyika kuanzia tarehe leo tarehe 6-10 mwezi huu katika viwanja vya Karimjee na viwanja vya Mwalimu Nyerere (sabasaba).
Mkaguzi Mkuu wa ndani kutoka Wizara ya Fedha na Mipango Bw.Emmanuel Kizigha akihakiki nyaraka za mstaafu anaelipwa na Wizara ya Fedha na Mipango,uhakiki huo unafanyika kuanzia leo tarehe 6-10 Machi katika viwanja vya Karimjee na Sabasaba. Picha na Daudi Manongi-MAELEZO.