Uongozi wa Kampuni ya Reli Tanzania –TRL unachukua fursa hii kuwataarifu wateja wetu wote na Watanzania kwa ujumla na hasa maeneo ya kituo cha Reli cha Nguruka mkoani Kigoma, kuwa treni yetu maarufu ya Deluxe itasimama kituoni hapo kuteremsha na kupakia abiria.
Kwa taarifa hii ambayo ilikuwa ikisubiriwa kwa hamu na Wakazi wa maeneo yanayozunguka kituo cha Nguruka, shime wajitokeze kwa wingi kukata tiketi za safari kwa mujibu wa mahitaji yao .
Halikadhalika safari za deluxe zitakuwa wiki mara moja siku za Jumapili itaondoka Stesheni ya Dar es Salaam saa 2 usiku ikiwa na mabehewa yasiozidi 15, Daraja la kawaida 10 (abiria 80 kila moja) daraja la pili la kukaa 3 (kila moja abiria 60) na daraja la pili kulala 2( kila moja abiria 36).
Kwa sasa itasimama katika vituo 18 ambavyo ni pamoja na Morogoro, Kilosa, Dodoma, Makutopora, Saranda, Manyoni, Aghondi, Itigi, Tabora, Urambo, Kaliua, Nguruka, Uvinza, Kigoma. Vituo vingine ni Isaka, Shinyanga, Malampaka na Mwanza. Wiki moja ikienda Kigoma wiki inayofuatia itaenda Mwanza.
Kwa wasafiri wa Dodoma na Tabora hawa watatumia huo usafiri wakati wote isipokuwa wale wanaoishia Kigoma na Mwanza. Kuhusu mapendekezo ya safari za deluxe zianze saa 2 asubuhi, Uongozi wa TRL unalifanyia kazi pendekezo hilo na muda sio mrefu litapatiwa majibu.
NAULI ZA TRENI YA DELUXE KWA MUHTASARI KUTOKA DAR KWENDA KIGOMA/MWANZA NI KAMA IFUATAVYO:
Dar -Dodoma daraja la kawaida TZS 18,500, Daraja 2 Kukaa TZS 24, 700 na Kulala: 41,200
Dar -Tabora kawaida 25,400, Daraja la 2 Kukaa 33,900 na Kulala 56,500;
Dar – Nguruka kawaida 31,200 Daraja la 2 kukaa 41,600 na kulala 69,300
Dar - Kigoma kawaida 35,700, Daraja la 2 Kukaa 47,600 na Kulala 79,400 na
Dar - Mwanza ;kawaida : 35,000, Daraja la 2 kukaa 46,700 na Kulala 77,800.
Aidha pia tunapenda kutoa wito wa ushirikiano wa wananchi na wadau wote kutunza vitendea kazi na kwamba kila mmoja awe mlinzi wa mwenziwe. Tujiepushe na vitendo vya makusudi kuharibu mabehewa haya mazuri ndani na nje . Kuna msemo : KITUNZE KIDUMU’! Tukitunza vitendea kazi vitaweza kutoa huduma kwa muda mrefu na hivyo kuongeza tija na kupunguza matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi.
Imetolewa na Afisi ya Uhusiano ya TRL kwa Niaba ya
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji ,
Mhandisi Elias Mshana
Dar es Salaam – Mei 12, 2015