Mhe. Lamamra naye akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo yao. |
Mhe. Membe akiagana na Mhe. Lamamra mara baada ya mazungumzo yao. |
Na Mwandishi Wetu, Addis Ababa
Tanzania na Algeria zimekubaliana kuendelea kuimarisha ushirikiano uliopo kwa ajili ya maendeleo ya nchi hizi mbili.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa Algeria Mhe. Ramtane Lamamra walipokutana pembezoni mwa Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika (AU) unaoendelea mjini Addis Ababa, alisema kuwa Tanzania inayo mengi ya kujifunza kwa Algeria hususan katika sekta ya gesi na umeme kwani nchi hiyo imepiga hatua kubwa katika sekta hizo.
“Algeria ni moja ya nchi zilizopiga hatua kubwa kimaendeleo kupitia sekta ya gesi asilia na umeme hivyo tunapenda kupata utaalam huo ili mtufundishe namna ya kukuza uchumi wetu kupitia gesi” alisema Mhe. Membe.
Mhe. Membe aliongeza kuwa Tanzania ni moja ya nchi zenye utajiri mkubwa wa gesi asilia hata hivyo bado inakabiliwa na ukosefu wa utaalam wa namna ya upatikanaji na usafirishaji wa gesi hiyo ili kukuza uchumi wa nchi. Alieleza kuwa Tanzania inayo mengi ya kujifunza kutoka Algeria kwani ni nchi yenye uzoefu katika masuala ya upatikanaji na usafirishaji wa gesi asilia.
Katika hatua nyingine, Mhe. Membe alimuomba Mhe. Waziri Lamamra kuisaidia Tanzania kuzungumza na Serikali za Iran na Iraq ili ziweze kuifutia Deni Tanzania kama Algeria ilivyofanya mwaka 2012.
Kwa upande wake, Mhe. Lamamra alisema kuwa, Algeria ipo tayari kushirikiana kwa karibu na Tanzania katika Sekta ya Gesi na Umeme na tayari Waziri wa Nishati na Madini wa Tanzania, Mhe. Sospeter Muhongo alifanya ziara nchini Algeria mwaka 2013.
Aidha, aliongeza kuwa, wakati wa ziara hiyo baadhi ya makubaliano katika sekta hiyo yalisainiwa ambapo Mhe. Muhongo pia alipata fursa ya kutembelea Kampuni kubwa ya Sonatrach inayojishighulisha na masuala ya gesi nchini humo.
Alisema kuwa Waziri wa Nishati wa Algeria amefanya ziara nchini Tanzania mapema mwezi Januari, 2014 na kufikia makubaliano na Wizara husika kuhusu suala la gesi na umeme.
Kuhusu suala la deni la Iran na Iraq kwa Tanzania, Mhe. Lamamra alisema atalifikisha suala hilo atakapokutana na Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi hizo.“Ndugu yangu umefanya vizuri kulileta suala hili kwetu, hivyo nitalifikisha kwa wahusika ili kutafuta namna ya kulishughulikia” alisisitiza Mhe. Lamamra.
Sekta ya gesi nchini Algeria inachangia Pato la Taifa kwa asilimia 55 huku asilimia 98 ya wananchi wanapata nishati ya umeme kwa matumizi mbalimbali.