JANUARI 2, mwaka huu Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, ilitoa zuio la muda kwa Kamati Kuu ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kutojadili uanachama wa aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Mhe Zitto Kabwe katika kikao cha chake cha Januari 3, mwaka huu.
Januari 3, mwaka huu mahakama hiyo ilisikiliza hoja za mawakili wa pande zote mbili kuhusu maombi hayo mbele ya Jaji John Utamwa.
Januari 7, mwaka 2014, mahakama hiyo pia ilitoa amri kwamba Zitto asijadiliwe uana chama wake hadi kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa maamuzi.
Mhe Zitto alikuwa anatetewa na wakili Mhe Albert Msando na Chadema walikuwa wanawakilishwa na Mhe Tundu Lisu na Mhe Peter Kibatala.
Katika kesi ya msingi, Zitto amefungua kesi dhidi ya Baraza la Wadhamini la Chama hicho na Katibu Mkuu, Willbrod Slaa, akiiomba Mahakama itoe zuio la muda la Kamati Kuu kutojadili suala la uanachama wake hadi kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa maamuzi na mahakama hiyo.
Katika maombi yake, Zitto anaiomba mahakama kuiamuru kamati kuu na chombo chochote kisijadili uanachama wake hadi rufaa yake itakaposikilizwa katika Baraza Kuu la Chama.
Kadhalika, anaoimba mahakama imwamuru, Katibu Mkuu wa CHADEMA Dk. Wilbroad Slaa kumkabidhi nakala za taarifa na mwenendo mzima wa vikao vilivyomvua uongozi ili akate rufaa katika ngazi ya juu ya chama hicho.
Mhe. Zitto kupitia wakili wake Msando aliomba mahakama itoe zuio la muda la Kamati Kuu na vikao vingine vya chama kutojadili suala la uanachama wake hadi kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa uamuzi.
Akiwasilisha hoja zake wakili Msando aliomba zuio hilo litolewe hadi Zitto atakapopata nafasi ya kuwasilisha rufaa yake ya kupinga uamuzi wa kumvua uongozi katika chama, uliotolewa katika kikao kilichofanyika Novemba 12 mwaka 2013.
Wakili Huyo alidai endapo amri hiyo haitatolewa na Kamati Kuu ikamvua uanachama, Zitto atapata athari kubwa kuliko chama chenyewe kwa kuwa atapoteza nafasi yake ya ubunge na kushindwa kuwatumikia wananchi waliomchagua.
Pia, mwanasheria huyo alidai athari nyingine ni kwamba iwapo atafukuzwa uanachama, Zitto atapoteza nafasi ya Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).
Alisisitiza kuwa, Zitto haizuii Chadema kufanyakazi zake za kisiasa kama wao wanavyodai katika hati ya kiapo kinzani, bali anaomba Kamati Kuu isijadili suala lake la uanachama mpaka uamuzi utakapotolewa.
Akijibu hoja hizo Wakili wa Chadema, Mhe Lissu alidai kuwa katika kutoa zuio la muda mahakama inatakiwa iangalie maslahi ya walio wengi na si faida ya watu wachache.
Alidai katika hati ya kiapo, Mhe Zitto anadai hakuna tarehe ya kikao cha Baraza Kuu la chama kilichopangwa, pia asipokata rufaa hatotendewa haki na atapata madhara lakini dawa ya woga na hofu yake ni kuomba mahakama iamuru kikao cha Baraza Kuu kifanyike na siyo kuomba zuio.
Mhe Lissu alidai kuvuliwa uanachama kwa Zitto hakutakuwa na athari kubwa kama anavyodai, na kwamba athari atayoipata yeye ni kukosa posho na mishahara.Baada ya kurejea vifungu mbalimbali vya sheria, kanuni, amri na uamuzi wa kesi mbalimbali za Mahakama Kuu, Mahakama ya Rufani na za nje, Jaji Utamwa alisema anakubaliana mtoa maombi.
“Kwa hiyo ninatoa zuio la muda kwa Kamati Kuu ya Chadema na au chombo chake chochote cha uamuzi kwamba kisimjadili na kutoa uamuzi wowote dhidi ya mleta maombi kuhusiana na uanachama wake kusubiri kusikilizwa na kuamuriwa kwa kesi yake ya msingi,” alisema Jaji Utamwa.
Kesi ya msingi inatarajiwa kutajwa Februari 13, mwaka huu.