Na Moshy Kiyungi
Mwanamuziki Ramadhani Masanja ‘Banza Stone’ alikuwa mahiri kwa utunzi pia uimbaji wake katika bendi mbalimbali alizowahi kuzifanyia kazi.
Kabla ya kifo chake baadhi ya watu walikuwa wakimzushia kifo mara kwa mara kuwa amefariki dunia.
Lakini uzushi huo ukageuka kuwa ukweli Julai 17, 2015, alipoiaga dunia akiwa nyumbani kwao Sinza jijini Dar es Salaam.
Julai 18, 2015, taratibu zote za dini ya Kiislamu zilifanywa, Ramadhani Masanja ‘Banza Stone’ akawekwa kwenye nyumba yake ya milele katika makaburi ya Sinza jijini Dar es Salaam.
Banza Stone kabla ya kifo chake maradhi makali yaliyopelekea kulazwa katika hospitali ya Mwananyamala, kutokana na ugonjwa wa saratani ya ubongo.Aliwahi kuwalalamikia mara kadhaa baadhi ya watu waliokuwa wakimzushia kifo, akisema anajisikia vibaya sana na si jambo jema kuzushiwa kifo.
Banza akizungumza kwa taabu alitamka kwamba alitamani apone ili arudi tena jukwaani, akisema kuwa maombi yao ni muhimu na msaada mkubwa kuliko kitu chochote.Wasifu wa Banza unaeleza kuwa alizaliwa katika hospitali ya Ocean Road, jijini Dar es Salaam, Oktoba 20, 1972 akiwa ni mtoto wa tisa kati ya 11 katika familia yao.
Alipata elimu ya msingi katika shule ya Mnazi mmoja jijini Dar es Salaam na alifanikiwa kumaliza darasa la saba mwaka 1987. Banza baada ya kumaliza shule, alianza taratibu za kujihusisha na maswala ya muziki akiwa angali mdogo.Alijiunga katika muziki wa Hip Hop uliokuwa ukisikika katika redio.
Masanja aliwahi kunukuliwa akisema kuwa “…mara tu baada ya kumaliza elimu yangu ya msingi, nilianza kujihusishana muziki wa Hip Hop, enzi hizo tulikuwa tukisikia katika redio, pia tukienda dansi tunakuta nyimbo za wasanii kadhaa wa Hip Hop zikirindima.
Wakati huo nilikuwa na wenzangu kama kina K One na Scoz Man…” alisema Banza.Banza alieleza kuwa wakati huo ilikuwa vigumu sana kupata nafasi ya kutumbuiza eneo lolote lile kwani muziki huo hakukubalika.Alikumbuka mwishoni mwa mwaka 1989, walikuwa wakienda Coco Beach kuonesha vipaji vyao vya kuimba muziki wa Hip Hop.
Banza alitamka kuwa vijana wengi walionesha kuukubali muziki huo japo ilikuwa ngumu sana kueleweka mbele ya jamii kutokana na muziki huo wa Hip Hop kuonekana kama uhuni.“Tulikuwa na kazi kubwa ya ziada kufanya vile inavyotakiwa, lakini bahati haikuwa yetu wazazi walileta kipingamizi.
Hata hivyo tulionekana kama vijana wa kihuni….” anasikitika Banza Stone.
Japo alipenda sana muziki, wazazi wake waliweka pingamizi baada ya kuonekana muziki huo wa Hip Hop kuwa ni wa kihuni.
Mwaka 1990 akaamua kuanza mchakato mpya wa ‘kunengua’ muziki wa dansi, ambapo alikuwa akicheza kwenye harusi na kufanikiwa kupata fedha kidogo.
Mwaka 1995 Banza alijiunga katika bendi iliyochini ya Kampuni ya African Stars Entertainment Tanzania (ASET) ya Twanga Pepeta kabla ya kuchepukia katika bendi ya Extra Bongo iliyokuwa ikiongozwa na Alli Choki.
Banza alionesha kupevuka kifikra mwaka 2000, alipomua kwenda kupata mafunzo ya muziki sehemu tofauti ikiwemo Kituo cha Utamaduni cha Watu wa Korea.
Aidha alipokuwa katika bendi ya Tanzania One Theatre (TOT), wanamuziki wake walipelekwa kuapata mafunzo hayo katika Chuo cha Sanaa Bagamoyo akiwemo yeye.
Baada ya kuhitimu alianza kuimba katika bendi mbalimbali zikiwamo za The Heart Strings, bendi za Twiga na Achigo, akiwa mpiga ngoma pamoja na Afri-Swez na zingine ndogo ndogo.
Katika bendi hizo zote hizo alikuwa akidumu kwa miezi kadhaa, kabla ya kuhamia katika bendi nyingine hadi alipoingia katika bendi ya The African Stars, “Wana Twanga Pepeta” akawa na ahuweni ya maisha.
Soko la Banza lilikuwa kubwa hivyo baada ya kuipaisha Twanga Pepeta kwa kiasi kikubwa, alichukuliwa kwenda kujiunga katika kundi la Tanzania One Theatre (TOT) “Wana Achimenengule”
Akiwa hapo alijulikana zaidi kwa jina la ‘Mwalimu wa Walimu’ japo nako hakukaa sana.Ramadhani Masanja ‘Banza Stone’ aliamua kuanzisha bendi yake iliyokuwa ikiitwa Bambino Sound.Kwa bahati mbaya bendi hiyo ilidumu kwa miezi kadhaa kabla ya kusambaratika kutokana na uongozi mbovu.
Banza aliwahi kuelezea kwamba katika kipindi cha miaka 23 tangu aanze muziki wa dansi rasmi, haikuwa rahisi kwake kupata mafanikio mazuri licha ya kuzunguka sana kutafuta maisha.Banza Stone alipitia zaidi ya bendi tisa ikiwemo Rufita Band.
Mwaka 2014, msanii wa muziki wa kizazi kipya, Hamisi Ramadhani ‘H-Baba’ alimshirikisha Banza kurekodi wimbo wake mpya wa ‘Sina Raha’.Kibao hicho kimo kwenye albamu mpya ya msanii huyo inayojulikana kwa jina la ‘Shika Hapa, Acha Hapa’.
Banza Stone hatunae tena hapa duniani, lakini ametuachia ujumbe mzito kutoka kupitia nyimbo zake ambazo bado zitamba.Baadhi ya nyimbo hizo ni za Mtaji wa Maskini, Kumekucha, Elimu ya Mjinga, Angurumapo Simba Mcheza nani na Falsafa ya Maisha.
Ramadhani Masanja alikuwa ‘msanii wa ukweli’ kwani alithubutu kuimba vibao kadhaa vya taarabu ukiwamo ‘Kuzaliwa mjini’ na ule wa ‘Play Boy’.
Banza alieleza jinsi alivyohangaika ili kufikia kuwa msanii mkubwa hadi kujulikana.Alisema alifanya subira ili kutimiza doto zake zilizokuja hatua kwa hatua.
Mwaka 1990 waliamua kuanza mchakato mwingine wa kunengua akiwa na wenzake wakicheza hususan kwenye harusi mbalimbali, wakaweza kupata fedha kiasi.Banza alifafanua kuwa walikuwa wakifanya maonesho kwa muda mrefu kidogo na wakati huo walikuwa wakicheza kwa kufuatisha nyimbo za wanamuziki kutoka nje, kama wa Michael Jackson na wengine.
“Mwaka 1995 niliingia Twanga Pepeta, wakati huo bendi hiyo ilikuwa bado changa sana, tulianza kwa kutoa albamu ya “Kisa Cha Mpemba”
Bendi hiyo ikaendelea kukua zaidi kimuziki mpaka kufikia katika hatua ya kuwa bendi bora ya muziki wa dansi nchini mwishoni mwa miaka ya 1990…” alitamka Banza.Ramadhan Masanja kuna kipindi alivuma mno kwa wimbo wa Kumekucha, uliokuwa wa kwanza kutunga na kurekodi studio mwaka huohuo.
Alisema hapo ndipo safari ya muziki ilipoanza, aliamua kuendelea na shule ya muziki baadae mwaka 2000, ili kuongeza ujuzi na maarifa katika kazi yake.Baadae aliicha bendi ya Twanga na kutimkia katika bendi Tanzania One Theater (TOT Plus) ambako nyota yake ilizidi kung’ara.
Akiwa TOT Plus, alishirikiana na wakali wengine wakiwepo Abdul Misambano, Papii Kocha na wengine wengi waliosababisha kuwepo upinzani mkubwa wa kimuziki dhidi ya Twanga Pepeta.
Banza alitua TOT Plus 1999 chini ya ukurugenzi wa Kapteni John Komba ambaye alimchukua mwimbaji huyo ili kuliimarisha kundi hilo liweze kupambana na Twanga Pepeta.Wakati huo ndipo Banza alipotoa ‘rap’ mpya wa ‘Uliona wapi Tingatinga likaenda kwenye starehe’ kikiwa ni kijembe kwa rafiki yake wa karibu Ally Choki ambaye wakati huo alikuwa Twanga Pepeta.
Kuna siku Choki katika uzinduzi wa moja ya albamu, aliingia katika ukumbi wa Diamond Jubilee akiwa juu ya Kijiko au Tingatinga.Mbali ya rap hiyo akiwa TOT, Banza pia alitunga vibao kama Elimu ya Mjinga ni Majungu, Mtaji wa Maskini Nguvu zake mwenyewe, Angurumapo na Simba sehemu ya pili.
Mwaka huohuo Banza alirejea katika bendi ya African Stars ‘Wana Twanga Pepeta’ ambako alikutana na Alli Choki pamoja Luiza Mbutu chini ya uongozi wa mkurugenzi Asha Baraka, ilipoedelea kupata umaarufu mkubwa zaidi.
Nyimbo za Angurumapo Simba, Kisa cha Mpemba, Mtaji wa maskini, Elimu ya Mjinga, Mtu na Pesa zake na nyingine nyingi zilizovuma na kuipa umaarufu bendi hiyo ni kielelezo halisi cha uwezo aliokuwa nao marehemu Banza Stone.Hakika kifo chake kilileta simanzi kubwa kwenye tasnia hiyo.
Huko Africana Stars Banza Stone alijulikana zaidi kwa jina la ‘Mwalimu wa Walimu’ japo hakukaa kwa muda mrefu katika bendi hiyo.Baadae mwanamuziki huyo aliondoka TOT Plus na kwenda kuanzisha kundi lake la Bambino Sound.Akiwa na bendi hiyo, alitoka na kibao cha ‘Mimi niseme na wewe Useme nani atamsikiliza mwenzie?
“Bendi yangu ilikuwa inaitwa Bambino Sound, ambayo ilidumu kwa miezi kadhaa tu, lakini ilivunjika kutokana na kutokuwa na uongozi mzuri, haikuwa na mtu makini hilo ndilo liliangusha bendi hii, hatimae nikarudi tena African Stars Band. Baadaye nilienda Extra Bongo…” alisema Banza katika mahojiano wakati wa uhai wake.
Bendi hiyo haikudumu kwa kipindi kirefu, ikafa.
Banza Stone alikuwa , mtunzi, mwimbaji na rapa wa muziki huo nchini. Pia alianika idadi ya bendi alizopitia katika kipindi cha miaka 23 tangu aanze muziki wa dansi rasmi.Aliweka wazi kwamba alipita kupiga muziki katika bendi zaidi ya bendi tisa, katika harakati zake za za muziki.
Banza aliwahi kutunga na kuimba nyimbo akiwa katika bendi ya Twanga Chipolopolo na Rufita Jazz kabla ya kujiunga na Extra Bongo, inayoongozwa na Ally Choki.
Akiwa na Extra Bongo, Banza alikuwa akitamba na kibao chake kinachojulikana kwa jina la ‘Falsafa ya Maisha’. Pia alikuwa akiimba nyimbo alizowahi kutamba nazo katika bendi mbalimbali.
Mwaka 2003 Banza alikuwa miongoni mwa wanamuziki watatu nguli nchini, wengine Ally Choky na Muumini Mwinjuma, walioibuka na zing zong yao iliyoandaliwa na Mohamed Mpakanjia (sasa marehemu).
Mwaka mmoja baadae alirejea tena Twanga Pepeta na kuibuka na kitu kikali kilichojulikana kama ‘Mtu Pesa’.Kabla hakijapoa, akiachia tena kibao cha ‘Hujafa hujasifiwa’, ambacho alisema alitunga baada ya mara kadhaa kuzushiwa kifo.Nguli huyo alisema kuwa alikwisha rekodi vibao kadhaa alivyoimba kwa mtindo wa Hip Hop, kati ya hizo upo wimbo alioutengeneza akiwa na Chid Benz miaka miwili iliyopita ambao hakufanikiwa kuutoa.
“Nina wimbo ambao haujatoka, lakini nimesha achia wimbo mmoja Mshenga, niliorekodi na Man Dojo na Domo Kaya ambao haukufanikiwa kufanya vizuri katika chati za muziki wa kizazi kipya…” alitamka Masanja Banza Stone.
Wimbo mwingine aliorekodi ni Sema unachotaka, aliouimba akishirikiana na Godzilla ambao alipanga kuupeleka redioni mwaka huo.
Marehemu Banza atakumbukwa kwa mengi kutokana na umahiri wake wa kutunga na kuimba na kutunga nyimbo ambazo ‘ziliwabamba’ mashabiki wa muziki huo na kujikuta akiwa kipenzi cha watu wengi wa muziki wa dansi.
Msanii mwenzake aliyefanya nae kwa ukaribu, Ally Choki alisema kuwa Banza Stone alikuwa na kipaji cha kipekee na alikuwa chachu kubwa ya kukua kwa muziki wa dansi tangu alipojitumbukiza kwenye tasnia hiyo 1991 akianzia kama mnenguaji kwenye kundi la Sinza Stars.
Alikiri kuwa kuna kipindi Banza aliwahi kuwa mpinzani wake mkubwa wa kwenye ushindani katika muziki, licha ya kuvutiwa na uimbaji wake.
Hali hiyo Choki alilazimika kufanya mazoezi ya ziada ili aweze kuhimili ushindani kutoka kwa mkali huyo ambaye nyota yake imezimika ghafla.
Banza aliwahi kuimba vibao kadhaa vya taarabu ukiwamo Kuzaliwa Mjini na ule wa Play Boy.
Licha ya kuwa msanii bora wa muziki wa dansi Banza Stone alisema, “…nashindwa kukua zaidi katika muziki kutokana na maradhi yanayonisumbua, muda mwingi ninakuwa kitandani, hivyo nashindwa kuendelea vizuri katika kazi zangu, kipindi cha hivi karibuni nilipumzika muziki kwa miezi kadhaa lakini Mungu mkubwa kwani hivi sasa ninaendelea vizuri…”
Banza baada ya kupata ahuweni alitarajia kurejea tena katika bendi yake aliyokuwa akiitumikia ya Extra Bongo na kufanya mambo makubwa zaidi.
“Natarajia kufanya kazi ambayo mashabiki watafurahia, tumeshazindua albamu ya ‘Mtenda Akitendewa’ na ‘Kinachosubiriwa’ hivi sasa ni kazi mpya, tayari nina vibao kadhaa ambavyo vitatoka mapema mwaka huu...” alisema Banza Stone.
Ni dhahiri kwamba Banza Stone ameacha alama katika muziki wa dansi hapa nchini kupitia nyimbo zake zitakazoendelea kuishi na kuwa kumbukumbu na elimu kwa jamii.Kabla ya kulazwa hospitalini Banza tayari alikuwa amekwisha kata tama ya kuishi kwa vile aliwahi kuota ndoto kuwa mwisho wake wa kuishi duniani umekaribia.
Alieleza kwamba aliota ndoto anakufa na ameoneshwa jinsi kifo chake kwamba ataugua ghafla na kufariki dunia.Nyota huyo alisema kufuatia ‘maono’ hayo, ameanza kutunga nyimbo ambazo zingezungumzia historia ya maisha yake.“Ni kweli naona mwisho wangu umekaribia, nimeoneshwa ndotoni, inawezekana ni mpango wa Mungu ili nitengeneze maisha, nimeshaanza kuandaa albamu itakayohusu historia ya maisha yangu…” alisema Banza
Stone. Alizidi kusema kwa masikitiko kuwa baada ya ndoto hiyo amekosa raha ya kuishi tena na hajui yupo katika ulimwengu upi, kwani anafikiria maisha ya ulimwengu mwingine atakaoelekea.Banza alisema kwamba ndani ya moyo wake ana siri nzito ambayo angeitoa kwenye moja ya nyimbo zake hizo.
“Yaani mawazo yangu hayapo hapa, sijui niko dunia gani, nimekata tamaa, ninauona mwisho wa maisha yangu upo karibu lakini siogopi, natamani kufa kwa sababu ni lazima nitakufa hata nikiishi miaka mingapi…” alisema Banza.Mwaka 2014, Nyota huyo aliugua kwa muda na kulazwa kwenye Hospitali ya Mwananyamala, jijini Dar es Salaam.
Habari za mara kwa mara zilikuwa zikizushwa kuwa amefariki dunia, lakini siku yake ilipowadia, Julai 17, 2015 Ramadhani Masanja ‘Banza Stone’ akaaga dunia.Julai 17, 2019, Banza Stone atatimiza miaka minne tangu aiage dunia.
Mungu uiweke roho yake pahala pema peponi, Amina.