Na Leandra Gabriel, Blogu ya jamii
ALIYEKUWA Askofu Kanisa Katoliki la Virginia magharibi nchini Marekani Michael J. Bransfield (75) anadaiwa kutumia fedha za Kanisa kwenye mambo ya anasa ikiwemo pombe, kusafiri, kutoa zawadi kanisani, na kukarabati kanisa huku pia akikabiliwa na tuhuma za kuwadhalilisha kingono watu wazima wakati akiongoza kanisa hilo.
Kwa mujibu wa jarida la Newyork Post la nchini humo limeeleza kuwa askofu huyo ametumia kiasi kikubwa cha fedha za kanisa kwa matumizi binafsi na ya anasa tofauti na sheria na kanuni za kanisa hilo.
Imeelezwa kuwa Bransfield ametumia dola za kimarekani 350,000 kwa kutoa zawadi kanisani, dola milioni 2.4 kwa kusafiri pekee pamoja na huduma za hoteli, dola 1000 kwa matumizi ya pombe, dola milioni 4.6 kwa kukarabati kanisa na matumizi ya kuleta maua ofisini kwake kila siku yaliyogharimu dola 182, 000.
Alipohojiwa na jarida hilo kuhusiana na tuhuma dhidi yake Bransfield aliesema kuwa kila mtu anajaribu kumchafua na kueleza kuwa watu hao ni hatari sana na hakuwa wazi aliwalenga watu gani.
Uchunguzi dhidi tuhuma hizo dhidi ya Askofu Michael Bransfield uliongozwa na Askofu mkuu William Lori wa Baltimore.
Bransfield alikuwa Askofu wa Kanisa hilo tangu mwaka 2005 na alilazimika kuachia ngazi hiyo Septemba, 2018 baada ya Baba Mtakatifu Francis kutangaza uchunguzi dhidi yake.