WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola ameliagiza Jeshi la Polisi Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, kuhakikisha wamewakamata wahusika wa mauaji ya watu wanane yaliotokea mwezi mmoja uliopita katika Kata ya Kitanga yaliosababishwa na mgogoro wa wakulima na wafugaji kijijini humo.
Akizungumza na mamia ya wananchi wa Kijiji cha Kitanga wilayani humo, jana, Waziri Lugola alitoa siku mbili kwa Jeshi hilo kukamilisha kazi hiyo kwa kufanya operesheni maalum ili kuondoa taharuki kwa wakazi wa eneo hilo.
“Lazima tupendane, kwanini tunauana, wasukuma na waha wote ni ndugu, tushirikiane, tupendane ili tuweze kuishi kwa Amani, hizi chuki nataka ziishe, mkuu wa wilaya shirikiana na polisi ili hili tatizo liweze kuisha haraka iwezekananavyo.,” alisema Lugola.
Waziri Lugola aliongeza kua, katika siku mbili alizotoa anataka watuhumiwa wote wawe wamekamatwa na kushtaki kwa mauaji ya watu wanane.
Huku akiwa anashangiliwa na wananchi hao, Lugola alisema Serikali itaendelea kuwalinda wananchi wake kwasababu Tanzania ni nchi ya Amani na pia watu wake wana upendo.
Lugola pia alimtaka Mkuu wa Wilaya wa Kasulu…..kupitia Kamati yake ya Ulinzi na usalama ihakikishe wanatoa maeneo ya wafugaji na pia marufuku kwa wafugaji hao kuingiza mifugo mashambani.
“Mkulima haupaswi kwenda kulima sehermu ya malisho ya mifugo, halikadhalika wafugaji marufuku kuingiza mifugo yenu katika eneo la wakulima, huo ni utaratibu mzuri, tuufuate na tuzingatie ili kuimarisha Amani katika eneo hili,” alisema Lugola.
Aidha, katika hatua nyingine Waziri Lugola alizungumza na wananchi wa mji wa Kasulu na kusema Serikali inaangalia uwezekano wa kuandaa vibali maalum vitakavyoruhusu wakulima wa wilaya hiyo kuwatumia vibarua kutoka nchi za Burundi na Kongo ili kupunguza wahamiaji haramu wanaokuja mkoani Kigoma kufanya kazi za kilimo ambao baadhi yao si waamini.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola akizungumza na wananchi wa Kata ya Kitanga, Wilaya ya Kasulu, Mkoani Kigoma wakati alipofanya ziara katika kata hiyo kwa ajili ya kuzungumza na wananchi baada ya kutokea mauaji katika eneo hilo yaliyotokana na vurugu ya wakulima na wafugaji mwezi uliopita. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kushoto) akimsikiliza mwananchi wa mjini Kasulu alipokua aamuuliza maswali, baada ya Waziri huyo kuwataka wakazi wa mji huo kutoa kero mbalimbali zinawakabili wilayani humo. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kulia), akimsikiliza Mkazi wa Kijiji cha Kitanga, Shabani Funyenge, alipokua anamfafanulia jinsi ugomvi wa wakulima na wafugaji ulivyoanza katika Kijiji hicho, Wilaya ya Kasulu, Mkoa wa Kigoma, uliosababisha watu wanane kuuawa. Lugola alitoa siku mbili kwa watuhumiwa wa mauaji hayo wawe wamekamatwa. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.