Na Humphrey Shao Globu ya Jamii
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa hesabu za Serikali (CAG) Prof. Mussa Assad, amesema Tanzania ni moja ya nchi zinazofanya vizuri katika bara la Afrika na kushika nafasi ya tatu kwa bara zima.
Profesa Assad amesema hayo leo jijini Dar es Salaam mara baada ya kurejea nchini akitokea nchini Marekani kukabidhi nafasi ya ujumbe wa bodi ya ukaguzi ya Umoja wa Mataifa (UNBoA) kwa nchi ya Chile baada ya Tanzania kumaliza kipindi chake cha miaka sita iliyoanza Julai mosi 2012
Makabidhiano hayo yamefanyika jana kwenye Ukumbi wa Mikutano uliopo kwenye jengo la Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York nchini Marekani na Tanzania kumaliza kupongezwa kwa kazi nzuri iliyofanya
Pamoja na kufanya makabidhiano hayo, CAG Prof. Assad pia alihudhuria Kikao cha kawaida cha 72 cha bodi hiyo na kuwasilisha jumla ya ripoti 13 za Ukaguzi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN)
Ripoti alizowasilisha baada ya kutiwa saini na wajumbe wa bodi ya UN ni pamoja na Ukaguzi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP), Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu Duniani (UNFPA), Shirika la Umoja wa Mataifa la Misaada kwa Wakimbizi wa Palestina na Mashariki (UNRWA), Mfuko wa Akiba kwa Watumishi wa UNRWA Wakazi (UNRWA – SPF), Shirika la Umoja wa Mataifa la Masuala ya Wanawake (UN – Women) na Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Mazingira (UNEP).
Ripoti nyingine ni za Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Mazingira ulio chini ya UNDPGEF, Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Mazingira ulio chini ya Shirika UNEP-GEF, Mfuko wa Mikopo Midogo midogo ulio chini ya UNRWA - MD Shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi (UN Habitat), Shirika la Umoja wa Mataifa la Ukuzaji Mitaji (UNCDF), Mahakama ya Umoja wa Mataifa inashughulikia Mauaji ya kimbari ya Yugoslavia ya zamani (ICTY), pamoja na ripoti ya Mpango wa Kupunguza Shughuli za Mahakama za Kimataifa zinazoshughulikia Mauaji ya Kimbari (MICT).
Prof. Assad amesema Tanzania itaendelea kuwa mjumbe mwangalizi ”Observer Member” kwenye Jopo la Wakaguzi wa Nje wa Umoja wa Mataifa kwa kipindi cha miaka miwili mfululizo baada ya kung’atuka kwenye nafasi ya Ujumbe wa bodi hiyo.Amesema katika kipindi cha miaka sita mbali ya kuwa mjumbe wa bodi ya UNBOA,pia Tanzania ilipata fursa ya kuongoza bodi ya Ukaguzi wa umoja wa Mataifa kwa kipindi cha miaka miwili,
Nimekuwa mwenyekiti wa UNBoA kwa miaka miwili mfululizo kuanzia Januari Mosi, 2015 hadi 31 Desemba, 2016, ambapo nimekuwa na jukumu la kuwasilisha taarifa za UNBoA katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kupitia Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa”alisema
Tanzania inaingia katika historia ya dunia kuwa nchi ya kwanza katika Ukanda wa Afrika Mashariki na ya tatu (3) Barani Afrika kuteuliwa mjumbe wa Bodi ya Ukaguzi wa Umoja wa Mataifa (UNBoA) tangu kuanzishwa kwa Bodi hiyo mwaka 1946. Nchi nyingine za Afrika ambazo zimewahi kuwa wajumbe wa Bodi ya Ukaguzi ya Umoja wa Mataifa ni Ghana na Afrika ya Kusini tu.
Mdhibiti Mkuu na Mkaguzi wa esabu za Serikali .Profesa Mussa Assad akizungumza na Waandishi wa Habari mara baada ya kurejea kutoka kwenye Mkutano wa Baraza la ukaguzi la Umoja wa Mataifa
Waandishi wa Habari wakimsikiliza Mdhibiti Mkuu na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali .Profesa Mussa Assad mara baada ya kurejea kutoka kwenye Mkutano wa Baraz la ukaguzi la Umoja wa Mataifa