Na Anitha Jonas – WHUSM
Serikali imetoa pole kwa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo kwa kumpoteza Mwalimu mahiri John Mponda aliyekuwa balozi wa tasnia ya Sanaa nchini.
Kauli hiyo imetolewa leo na Naibu Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza katika ibada ya kumuaga marehemu huyo iliyofanyika katika Chuo cha TaSUBa Wilayani Bagamoyo kwa ajili ya kumuaga kwani anatarajiwa kuzikwa kijiji cha Mbalizi Mkoani Mbeya.
“Tunatambua mchango wa Mwalimu John Mponda katika tansia ya sanaa nchini na kupitia wanafunzi waliyopita katika mikono yake pamoja na vikundi vya vijana alivyovianzisha ambavyo amekuwa akivifundisha kazi za sanaa, hakika tumempoteza mtu makini,”alisema Mhe.Shonza.
Akiendelea kuzungumza katika msiba huo Mheshimiwa Shonza aliwasihi wasanii waliyopata mafunzo kutoka kwa mwalimu huyo kuwa mabalozi kwa wasanii wenzao na kuwashauri misingi iliyobora katika katika kukuza na kuendeleza kazi za sanaa.
Kwa upande wa Mkuu wa Chuo cha TaSUBa Dkt.Herbert Makoye alisema kuwa marehemu mwalimu Mponda ameondoka katika kipindi walichokuwa wanamuhitaji sana kwani kwasasa taasisi hiyo ipo katika maandalizi ya Tamasha la Utamaduni la Bagamoyo ambalo nilakimataifa na hufanyika kila mwaka na yeye alikuwa mratibu na mpaka mauti yanamfika alikuwa akiwa shughulikia maandalizi hayo.
“Kwa hakika msiba huu ni pigo kwa taasisi yetu na mwalimu huyu alikuwa kiungo miongoni mwetu na alifanya kazi yake kwa weledi na kujituma alikuwa ni mtu aliyeipenda kazi yake ,’’alisema Dkt.Makoye.
Naibu Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza akisaini kitabu cha maombolezo ya msiba wa aliyekuwa Mkufunzi wa Sanaa katika Chuo cha Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) marehemu Mwl. John Mponda leo kabla ya ibada ya kumuaga kwa ajili ya safari ya mazishi yanayotarajiwa kufanyika Mbalizi mjini Mbeya.