Na Karama Kenyunko,Globu ya Jamii
Msanii Wema Abraham Sepetu (28), Ameendelea kusota Rumande huku wasanii wenzake 13 aliokuwa akishikiliwa nao kituoni hapo wameachiwa kwa dhamana na kutakiwa kuwa chini ya uangalizi wa polisi na mahakama kwa kipindi cha miaka minne.
Miss Tanzania 2006 huyo anaendelea kushikiliwa kwa zaidi ya saa 72 kwa sasa kwa tuhuma za kukutwa msokoto mmoja wa bangi na kusubiri uchunguzi kukamilika .
Taarifa kutoka chanzo makini cha habari kinasema wema ad anashikiliwa kwa uchunguzi Zaidi na muda wowote wiki hii anaweza kufikishwa mahakamani.
Katika kesi hiyo iliyosikilizwa leo katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilisikilizwa na mahakimu wawili ambapo watuhumiwa nane wa mwanzo walipewa dhamana ya milioni kumi (10,000,000) kila mmoja na watakuwa chini ya uangalizi wa polisi kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Watuhumiwa hao ni Hamidu Salum Chambuso (Dogo Hamidu), Rajabu Salum, Romeo George Bangura (Romy jons), Cedou Madigo, Khalid Salum Mohamed (TID), Johana Johanenes Mathysen (Director Joan), Rachael Josephat (Rachel) na Anna Patric Kimario (Tunda).
Mbele ya Hakimu Mkazi , Huruma Shahidi washtakiwa walitakiwa kujibu maombi ya waleta maombi ambao ni upande wa Jamhuri yaliyowasilishwa chini ya kiapo kilichoapwa na Mrakibu Msaidizi wa Polisi ASP Dennis Mujumba wa kitengo cha dawa za kulevya.
Sehemu ya kiapo hicho inadai kuwa wajibu maombi hao wanajihusisha na madawa ya kulevya hivyo kutokana na tabia hizo kuwaachia huru katika jamii bila kuwadhibiti kunaweza kusababisha uvunjifu wa amani katika jamii.
Katika maombi hayo,upande wa Jamhuri uliiomba mahakama iwaamuru wajibu maombi (wasanii hao), kuweka dhamana ya kuwa na tabia njema kwa kipindi cha miaka mitatu na kuwamuru kuripoti katika kituo cha polisi cha kati kwa mwezi mara mbili kwa ajili ya kuangalia mwenendo wa tabia zao.
Aidha Jamhuri waliiomba mahakama itoe amri yoyote nyingine itakayowafanya wajibu maombi hao kuwa na tabia njema na kuachana na kujihusisha na madawa ya kulevya.
Upande wa utetezi uliokuwa ukiongozwa na wakili Albert Msando ulidai kuwa kifungu cha sheria 73B ambacho wasanii hao wameshtakiwa nacho hakuna sehemu inayoonyesha makosa ya uvunjifu wa amani na kwamba mtu anayejihusisha na madawa ya kulevya hawezi kuvunja amani.
Akitoa amri, Hakimu Shahidi amewaamuru wasanii hao kuwa chini ya uangalizi wa mahakama kwa muda wa mwaka mmoja, wametakiwa kuwekewa dhamana ya kiasi cha milioni kumi (10,000,000) kila mmoja na pia wawe chini ya ulinzi wa polisi kwa ili waweze kujirekebisha na iwapo watakiuka watarudhishwa mahakamani.
Aidha hakukubaliana na maombi ya kuwataka wasanii hao walipoti polisi kila mwezi mara mbili akisema kuwa watakuwa wakijiandaa.
Wasanii Ahmed Hashim (Petitiman), Said Masoud Linnah (Said Alteza), Nassoro Mohamed Nassoro Bakar Mohamed Khelef and Lulu Abbas Chalangwe (Lulu diva) walifikishwa mbele ya Hakimu Mfawidhi Cyprian Mkeha.
Katika amri zake, aliwataka wasanii hao kuweka dhamana ya kiasi cha shilingi milioni ishirini (20,000,000) kila mmoja na kutojihusisha na makosa ya dawa za kulevya kwa kipindi cha miaka mitatu na wanatakiwa kuripoti Kituo Kikuu cha Kati kwa mwezi mara mbili pamoja na kutakiwa wabadilike na kuacha kabisa matumizi ya dawa hizo.
Hadi Globu ya Jamii inaondoka katika viwanja vya mahakama hiyo, wasanii hao walikuwa wamekamilisha taratibu zote za mahakama na walikuwa wakisubiri kurudishwa polisi kumalizia taratibu kabla hawajaachiwa huru.
Watuhumiwa wa kesi ya dawa ya za kulevya wakishushwa ndani ya gari ya polisi katika mahakama ya hakimu mkazi kisutu.
Msanii wa muziki wa kizazi kipya Khalid Mohamed akiingia katika mahakama ya hakimu mkazi kisutu.
Watuhumiwa wa kesi ya dawa ya za kulevya wakiingizwa katika mahakama ya hakimu mkazi kisutu jijini Dar es Salaam.
Mama yake Diamond akiwa na familia yake wakifatilia kesi ya ndugu yao yao Peti Man wakuache.
Petman wakuache akiwa na watuhumiwa wenzie akiwa katika mahakama ya hakimu mkazi kisutu.
Wasanii wa muziki wa Bongo Fleva wakiwa katika mahakama ya hakimu mkazi kisutu.
Msanii wa bongo fleva Rachel akiwa na wenzie katika mahakama ya Hakimu mkazi kisutu