Na Benny Mwaipaja, WFM, Songwe
Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Prof. Adolf Mkenda, amewaonya mawakala wa forodha katika mpaka wa Tanzania na Zambia wa Tunduma/Nakonde kuacha Mara moja tabia ya kuwachelewesha madereva wa malori yaendayo masafa marefu kwa makusudi ili wapewe rushwa.
Prof. Mkenda ametoa onyo hilo katika mpaka huo wa Tunduma na Nakonde, baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa baadhi ya madereva wa malori waliodai wamekuwa wakicheleweshwa kuvuka mpaka huo kwa zaidi ya siku tatu hadi tano.
Wadereva hao wameeleza kuwa mawakala wa forodha wamekuwa wakiwaambia kuwa nyaraka zao zinazohusika na mizigo wanayosafirisha zimekuwa zilicheleshwa na kituo cha Forodha upande wa Zambia.
Hata hivyo Meneja wa Mamlaka ya Mapato Zambia (ZRA), Kituo cha Nakonde, Bw. Nase Lungu, amekana kuhusika na ucheleweshaji huo na baada ya ukaguzi wa moja ya nyaraka hizo ilibainika kuwa upande wa Zambia unatoa nyaraka hizo kwa wakati lakini zimekuwa zikifichwa na Mawakala wa Forodha upande wa Tanzania.
Wakitoa ufafanuzi wa tuhuma hizo, madereva hao wamesema kuwa mawakala wa forodha kwa muda mrefu wamekuwa wakiwaeleza kuwa mtandao wa intaneti wa Upande wa Zambia unaotumika kuchakata nyaraka zao uko chini, hivyo walitakiwa kutoa shilingi 10,000 kwa kila nyaraka ili “kurahisisha” kazi hiyo kwa kuwapa kitu kidogo maafisa wa forodha wa Zambia.
“Mawakala wengine wa forodha wana nyumba zao za kulala wageni hapa Tunduma kumbe wanatulazimisha kukaa hapa ili tulale kwenye nyumba hizo hali inayotutia hasara na wanatumia kutokujua kwetu kutudanganya kwamba mtandao uko chini wakijua hatuna uwezo wa kufuatilia huko Zambia” alieleza kwa masikitiko dereva mmoja
Baada ya kubaini uwepo wa vitendo hivyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Prof. Adolf Mkenda, ameagiza Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA upande wa Tunduma kuandika kibao chenye namba za simu za Mkuu wa TRA mpakani hapo zitakazotumiwa na madereva wanaocheleweshwa kwa makusudi kutoa malalamiko yao.
“Tunataka madereva mtumie siku moja tu kukamilisha nyaraka zenu ili muendelee na safari yenu vinginevyo tutadumaza biashara kati ya Zambia na Tanzania na pia tutaifanya Bandari yetu ya Dar es salaam kushindwa kuleta tija” aliongeza Prof. Mkenda
Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Prof. Adolf Mkenda (kushoto), akiwa pamoja na Mkuu wa wilaya ya Momba mkoani Songwe, Bw. Juma Irando (katikati), na maafisa kadhaa wa Wizara ya Fedha na Mipango na Wizara ya Viwanda, Biashara naUwekezaji, wakitoka katika Ofisi za Mkurugenzi wa Mji wa Tunduma kuelekea mpakani mwa Tanzania na Zambia eneo la Tunduma na Nakonde
Kaimu Afisa Uhamiaji Mfawidhi wa Kituo cha mpakani Tunduma/Nakonde, Bw. Tabaran Mzee (kulia), akiueleza ujumbe kutoka Wizara ya Fedha na Mipango na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji namna idara yake ilivyojiandaa kuanza kutoa huduma ya pamoja mpakani kati ya maofisa kutoka Zambia na Tanzania ambao watakuwa wakitumia ofisi moja kuwahudumia watu wanaotumia mpaka huo kuvuka kwenda kila upande wa nchi (Tanzania na Zambia) Makatibu Wakuu kutoka Wizara ya Fedha na Mipango na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, wakiwa pamoja na maofisa wa mamlaka ya Mapato kutoka Zambia wakiangalia hali ya biashara na uwekezaji katika Mpaka wa Tunduma na Nakonde ikiwa ni maandalizi ya kuanza rasmi kwa utoaji wa huduma wa pamoja kati ya nchi hizo mbili ili kuboresha mazingira ya biashara baada ya kusainiwa kwa mikataba ya kuanzishwa kwa huduma hiyo katika mpaka huo
Makatibu Wakuu kutoka Wizara ya Fedha na Mipango na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, wakiwa pamoja na maofisa wa Mamlaka ya Mapato kutoka Zambia (ZRA) walipotembelea upande wa pili wa mpaka huo-Nakonde ili kujionea maandalizi ya kuanza rasmi kwa Kituo cha Pamoja cha Mpakani kati ya Tanzania na Zambia baada ya kusainiwa kwa makubaliano ya kuanzishwa kwa huduma hiyo Februari mosi, 2017
Ujenzi wa Kituo cha Pamoja Mpakani upande wa Tanzania-Tunduma, ukiendelea kwa kasi na una tarajiwa kukamilika baada ya miezi 16 ijayo
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-WFM)