Quantcast
Channel: MICHUZI BLOG
Viewing all 109593 articles
Browse latest View live

Miji Sita ya Zanzibar Kufanyiwa Mipango ya Matumizi ya Ardhi Ifikapo 2020

0
0
Na. Lilian Lundo – MAELEZO.

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) inatarajia kukamilisha upangwaji wa matumizi ya ardhi kwa ajili ya maboresho ya  Miji Sita ifikapo 2020.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira, Mhe. Salama Aboud Talib katika mahojiano na mwandishi wa habari hii kuhusu mafanikio ya Mkakati wa Matumizi ya Ardhi Zanzibar wa mwaka 2015.

Mhe. Salama amesema kuwa kumekuwa na mafanikio makubwa katika sekta ya  ardhi mara baada ya kuanzishwa kwa Idara ya Mipango Miji na Vijiji ambayo ilipelekea kuanzishwa kwa  mpango mkuu wa matumizi ya Ardhi uliosaidia kwenda kasi kwa shughuli za upangaji  wa matumizi ya ardhi ukilinganisha na miaka ya nyuma.

“Malengo ya Awamu ya Saba katika kupanga Miji ni kutengeneza mipango ya matumizi ya Ardhi (Master Plan) ya miji Mikuu miwili ambayo ni Zanzibar na Mji wa Chake-Chake na kufanya Mipango ya Maendeleo (Local Area Plan) ya miji midogo 14,” alifafanua Mhe. Salama.

Aliongeza kuwa kati ya miji Mikuu miwili, Mji wa Zanzibar umeshafanyiwa mipango ya matumizi ya ardhi na kati ya Miji 14, Miji 3 ya Nungwi, Chwaka na Mkokotoni imeshafanyiwa mipango yake.

Aidha amesema kuwa hadi kufikia mwaka 2020, Miji 6 itakuwa imefanyiwa mpango wa matumizi ya Ardhi. Aliitaja Miji hiyo kuwa ni Chake-Chake, Wete, Mkoa, Mkunduchi, Dunga na Mahonda.

Mhe. Salama amesema kuwa tangu  mwaka 1964 ni awamu hii ya saba ndiyo inayotoa kipaumbele katika masuala ya miji, ambapo taasisi maalum ya masuala ya miji imeundwa.

Pia kumekuwa na utekelezaji wa mipango ya matumizi ya ardhi ya mwaka 1968 ambayo imepata nguvu tena kwa kurudisha dhana adhimu iliyotungwa baada ya Mapinduzi ya kuwa na kitovu cha mji “Ngambo Tuitakayo”.

Waziri Mhagama azindua Bodi mpya ya NEEC

0
0
SERIKALI  imeridhishwa  na utekelezaji wa sera ya uwezeshaji wananchi kiuchumi na kuiagiza Bodi mpya ya Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) kufanya kazi karibu na watendaji baraza hilo ili kufikia malengo yake.

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu ( Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Bi.Jennista Mhagama, amesema serikali ina imani kubwa na bodi mpya ya Baraza na hivyo kulitaka kutekeza majukumu yake kwa uwazi na ufanisi.
 “Jukumu lenu kubwa ni kushauri na kuelekeza utendaji wa majukumu ya Sekretarieti ya Baraza ili waweze kuchochea Uwezeshaji unaotekelezwa na taasisi za umma na zile zile za binafsi,”alisema Bi.Mhagama wakati akizindua Bodi mpya ya Baraza juzi jijini Dar es Salaam.
Waziri Mhagama alisema kuwa Serikali inaimani kubwa Mwenyekiti na Wajumbe wote wa Baraza na pasipo shaka  uzoefu wenu katika masuala mbalimbali ya Uwezeshaji yataiwezesha Serikali kufikia ndoto yake ya kuona Mwananchi amewezeshwa katika maeneo yote muhimu hasa katika uchumi.
 ”Dhana nzima ya Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya mwaka 2004 ni kuona kuwa sehemu kubwa ya uchumi wa Tanzania inamilikiwa na watanzania wenyewe,” alisema na kuongeza kuwa jukumu la bodi ni kuhakikisha nafasi kubwa ya uwezeshaji inatolewa kwa makundi yote hasa yale yenye uwezo mdogo na kuwapa nafasi zaidi wanyonge.
 Alisema yote haya yanawezekana tukishirikiana kwa pamoja katika kutekeleza azma ya serikali ya kukuza uchumi imara kwa wananchi unaoweza kuhimili ushindani katika soko la dunia katika mazingira ya utandawazi.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Bi.Jennista Mhagama akisisitiza jambo katika kikao cha uzinduzi wa Bodi mpya ya Baraza la Uwezeshaji wananchi Kiuchumi(NEEC). Kulia kwake ni Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Dkt.John Jingu na kushoto ni katibu mtendaji wa NEEC,Bi.Beng’i Issa
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Bi.Jennista Mhagama akikabidhi nyenzo za kazi kwa Mwenyekiti wa bodi ya Baraza la Uwezeshaji wananchi kiuchumi(NEEC), Dkt. John Jingu katika kikao cha uzinduzi wa bodi hiyo mpya ya Baraza. 
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na W,alemavu Bi.Jenista Mhagama akikabidhi nyenzo za kazi mmoja wa wajumbe wa Bodi ya Baraza la Uwezeshaji wananchi kiuchumi(NEEC), Prof.Samuel Wangwe katika kikao cha uzinduzi wa Bodi mpya ya Baraza hilo.
Katibu Mtendaji wa Baraza la Uwezeshaji wananchi Kiuchumi (NEEC),Bi.Beng’i Issa akizungumza jambo katika kikao cha uzinduzi wa Bodi mpya ya Baraza hilo. Kulia kwake ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Bi.Jennista Mhagama na wapili kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya NEEC, Dkt. John Jingu.

Kamati ya gesi, mafuta Tanzania Bara, Zanzibar kuundwa

0
0
Na Greyson Mwase, Dar es Salaam.

Wizara ya Nishati na Madini kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Zanzibar zinatarajia kuunda Kamati Maalum kwa ajili ya kuandaa Mpango wa ushirikiano kati ya Tanzania Bara na Zanzibar katika sekta za gesi na mafuta.

Hayo yalielezwa mwishoni mwa wiki na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo katika kikao chake na Waziri wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Zanzibar, Salama Aboud Talib aliyeambatana na Ujumbe wake.

Wengine waliohudhuria kikao hicho ni watendaji kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA) na Mamlaka ya Udhibiti wa Shughuli za Mkondo wa Juu wa Mafuta (PURA).

Profesa Muhongo alisema lengo la kamati hiyo ni kujadili maeneo ya kushirikiana pamoja na kubadilishana uzoefu katika sekta za gesi na mafuta

Alisema kuwa, kamati hiyo itashirikisha Wataalam kutoka katika taasisi za Sheria, Ardhi, Kodi, Gesi na Mafuta chini ya Makatibu Wakuu wa sekta husika kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.Waziri Muhongo alisema kuwa, uwepo wa kamati hiyo utachochea Zanzibar kuwa na taasisi kama TPDC na nyingine hivyo kupelekea ukuaji wa sekta ya gesi na mafuta.

Alisisitiza kuwa, Serikali ya Tanzania Bara kupitia Wizara ya Nishati na Madini ipo tayari kushirikiana na Serikali ya Zanzibar pamoja na kubadilishana uzoefu katika masuala ya gesi na mafuta.Profesa Muhongo alishauri Serikali ya Zanzibar kuandaa wataalam wa mafuta na gesi kwa kuwasomesha katika ngazi za diploma na shahada katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo cha Madini Dodoma (MRI).

Akiongeza kuwa, Serikali ipo tayari kutoa ufadhili kwa wanafunzi wa Zanzibar wanaofanya vizuri katika masomo ya Sayansi kwa ajili ya kusomea shahada ya uzamili katika vyuo vya ndani na nje ya nchi.Naye Waziri wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Zanzibar, Salama Aboud Talib, alimshukuru Waziri Muhongo kwa utayari wa Wizara ya Nishati na Madini katika kushirikiana na Wizara yake kwenye shughuli za mafuta na gesi

Alisema kuwa, kamati itakayoundwa itapelekea mambo kwenda kwa kasi na kuwa na data za pamoja zinazotokana na utafiti wa mafuta na gesi na kupanga Mikakati ya kuvutia wawekezaji kutoka nje ya nchi.
Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Mhandisi Kapuulya Msomba ( wa tano kushoto, waliokaa mbele) akielezea majukumu ya shirika hilo katika kikao cha Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Waziri wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Zanzibar, Salama Aboud Talib aliyeambatana pamoja na ujumbe.
Mkurugenzi wa Mkondo wa Chini wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Dk Wellington Hudson akieleza jambo katika kikao hicho.
Kaimu Mkurugenzi wa Mkondo wa Juu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Venosa Ngowi akielezea shughuli za utafiti zinavyofanyika katika shirika hilo.
Kaimu Mkurugenzi wa Mkondo wa Juu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Venosa Ngowi akielezea shughuli za utafiti zinavyofanyika katika shirika hilo.
Kaimu Mkurugenzi wa Mkondo wa Juu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Venosa Ngowi akielezea shughuli za utafiti zinavyofanyika katika shirika hilo.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (katikati, waliokaa mbele) na Waziri wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Zanzibar, Salama Aboud Talib ( wa pili kutoka kushoto, waliokaa mbele wakiwa katika picha ya pamoja na watendaji kutoka Wizara husika.

Kamati za Umoja wa Walimu na Wazazi wa Shule za Msingi Zarudisha Nidhamu Shuleni.

0
0
Lilian Lundo - MAELEZO

Kamati za Umoja wa Walimu na Wazazi (UWW) katika Shule za Msingi za Serikali nchini zimefanikiwa kudhibiti utoro, nidhamu na kutofanya vizuri kwa baadhi ya Wanafunzi katika shule hizo kwenye mitihani yao ya kumaliza Elimu ya Msingi. Lilian Lundo wa Idara ya Habari (MAELEZO) anaelezea.

Mwaka 2015 Serikali kupitia Mpango wa Kuinua Ubora wa Elimu Tanzania (Education Quality Improvement Programme –Tanzania (EQUIP-T), ilianzisha Kamati za Umoja wa Walimu na Wazazi (UWW) katika shule za msingi nchini kwa lengo la kujenga uhusiano mzuri kati ya Walimu na Wazazi ikiwa ni njia mojawapo ya kuinua ubora wa elimu.

Aidha, Kamati hizo zilipewa jukumu la kufuatilia maendeleo ya Kitaaluma kwa Wanafunzi, kubuni miradi mbalimbali kwa ajili ya maendeleo ya shule na kubuni klabu mbalimbali ambazo zitawashirikisha Wananfuzi katika kujadili masuala ya kijamii na hivyo kuwavutia Wanafunzi kupenda masomo.

Mpango huo ambao awamu ya kwanza ulianza katika mikoa ya Dodoma, Kigoma, Lindi, Mara, Simiyu, Shinyanga na Tabora, umeleta mafanikio makubwa kimaendeleo ya kitaaluma darasani, kuongezeka kwa nidhamu na kudhibiti utoro jambo ambalo pia limeongeza ufaulu katika mitihani yao ya Elimu ya Msingi.

Kwa mujibu wa wa Mwalimu Mkuu wa Shule ya msingi Uhelela iliyoko Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma Bw. Dankan Kamwela, mpango huo umepata mafanikio makubwa katika shule yake ambapo imefanikiwa kupunguza utoro kutoka Wanafunzi 127 sawa na asilimia 30 kwa siku mwaka 2015 hadi Wanafunzi 12 sawa na silimia 8 kwa siku mwaka 2016.

Ameelezea kwamba, kwa kuitumia Kamati ya Umoja wa Walimu na Wazazi (UWW) wamekuwa wakifanya vikao mara kwa mara kwa kuwashirikisha Wazazi na Wanafunzi kujadili maendeleo ya Shule ikiwa ni pamoja na wajibu wa Walimu, Wazazi, na Wanafunzi kwa ujumla.

Amesema, kufuatia vikao hivyo ilibainika kuwa iko haja ya kuweka mikakati itakayosaidia kurekebisha kasoro zote zilizoonekana kuchangia kushuka kwa maendeleo ya kitaaluma, utoro na nidhamu ambavyo kwa pamoja vinasabisha kutofanya vizuri kwa Wananfunzi katika mitihani yao kwenye shule zilizo katika Kata hiyo. 

Kaya 227 za wafugaji Simanjiro zanufaishwa na mradi wa maji kutoka TanzaniteOne

0
0
Kaya 277 za wananchi 1767 wa Kijiji cha Losoito, Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wenye tatizo kubwa la ukosefu wa maji, wanatarajia kuondokana na changamoto hiyo baada ya kampuni ya TanzaniteOne kuwapatia maji.

Ofisa mahusiano wa kampuni ya madini ya Tanzanite ya wilayani humo TanzaniteOne Halfan Hayeshi alisema hivi sasa mradi huo umefikia asilimia 85 ili umalizike na kuzinduliwa ila wanachi wanapata maji.

Hayeshi alisema wananchi wa eneo hilo wanaendelea kupata huduma ya maji ila mradi kamili haujakamilika kwani wanahitaji kuweka mabomba urefu wa mita 500 ili kufikisha maji hayo karibu zaidi na jamii eneo la shule ya msingi Losoito.“Tunatarajia kuweka mabomba ya urefu wa mita 500 ili kufikisha mradi huu karibu zaidi, ila hivi sasa wananchi wanapata huduma hiyo ya maji kwani awali tuliambiwa tufikishe mradi huo kwenye eneo la sasa ulipo,” alisema Hayeshi.

Alisema wanatarajia kuzindua mradi huo hivi karibuni baada ya kuwapa taarifa Katibu tawala wa mkoa huo Eliakim Maswi na mkuu wa wilaya hiyo Zephania Chaula, ambao ndiyo wataukabidhi kwa wananchi wa kijiji hicho cha Losoito.Alisema mifugo na jamii ya eneo hilo hivi sasa wanafaidika na huduma hiyo ya maji na mara baada ya kununuliwa kwa rola sita za mabomba ya maji yatakayoweza kuwekwa katika mita 500 zilizobaki yatafika kwenye shule hiyo.

Ofisa mtendaji wa kijiji hicho Ngatayai Mollel alishukuru uongozi wa kampuni ya TanzaniteOne kwa kufanikisha mradi huo wa maji, utakaowasaidia wananchi wa eneo hilo, ambao kwa muda mrefu walikuwa wanakabiliwa na tatizo la maji.

Mollel alisema kijiji hicho kilichoanzishwa mwaka 2009 hivi sasa kina wakazi 1767 chenye kaya 277 kilikuwa na wakati mgumu wa kupata huduma ya maji ila hivi sasa wananchi wameondokana na changamoto ya maji iliyowasumbua.Hata hivyo, alitoa ombi la wananchi wa eneo hilo kujengewa zahanati kwani inawalazimu kutembea umbali mrefu kupata huduma ya afya pindi wanapougua hivyo kuwa tatizo hasa kwa wanawake na watoto.

Mmoja kati ya vijana wanaolinda mradi huo wa maji ili mabomba yasiibiwe Daniel Solomon, alisema wamepeana zamu ya kulinda kila siku watu watatu ili miundombinu isiharibiwe na jamii ya eneo hilo ifaidike na maendeleo hayo.

“Wakina mama walikuwa wanatembea umbali mrefu wa kilomita 20 kila siku kwenda na kurudi mji mdogo wa Mirerani, kwa kutumia wanyamakazi punda, ila hivi sasa wanaondokana na tatizo hilo la muda mrefu,” alisema Solomon.
Wakazi wa Kijiji cha Losoito Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wakiwa kwenye mradi wa bomba linalohifadhi maji yanayotumiwa na wanakijiji hao uliogharamiwa na kampuni ya TanzaniteOne, (kushoto) ni ofisa mahusiano wa kampuni hiyo Halfan Hayeshi.

KUMBILAMOTO ATETA NA WANA VINGUNGUTI JUU YA MAFANIKIO YA MWAKA MMOJA

0
0
Na Humphrey Shao, Globu ya Jamii

NAIBU Meya wa Manispaa ya Ilala na Diwani wa Vingunguti, Omary  Kumbilamoto amesema maisha ya watu wa vingunguti na uchumi wao inategemea pesa za biashara ya mbuzi.

Akizungumza na wakazi wa Vingunguti katika mkutano wa hadhara wa kueleza mambo aliyofanya ndani ya mwaka mmoja Kumbilamoto ametaja kuwa bila ya mbuzi vingunguti itakuwa maskini.

“nimejitahidi kutatua tatizo la wafanya biashara wa mbuzi ambao walitakiwa wahamishwe kupelekwa Pugu kwa kuangalia maslahi na vipato vya wakazi wa Vingunguti kuwa biashara hiyo itabaki vingunguti na itaendelea kama kawaida". amesema  Kumbilamoto.

Katika kipindi cha mwaka mmoja ambapo lengo lilikuwa kutoa shukrani, Kumbilamoto hakusahau Nyanja nyingine nyeti ikiwemo nyanja ya Afya ambapo alijitahidi kuwapatia Ambulance moja katika Hospitali ya Vingunguti ambayo ameahidi kuwa  mali ya wakazi wa  eneo hilo.

Pia hakuacha Elimu ambapo alisaidia shule ya Sekondari Miembeni kuchangia kupatikana kwa Umeme, hivyo wanafunzi kusoma bila matatizo , mambo mengine ambayo ameyagusia na kuyatolea ufafanuzi  ni pamoja na Sekta ya michezo, alitoa Mashine mbili za kufulia mashuka katika Hospitali hiyo, aliweza kushugulikia bomoa bomoa  na haki ya wafanyabiashara katika machinjio ambapo damu ilikuwa inapotea kwa wenye haki hawapati haki hiyo hivyo yeye amelishughulikia na limekaa sawa.
Naibu meya wa Manispaa ya Ilala na Diwani wa Vingunguti, Omary Kumbilamoto akiwa amekalia Cherahani mara baada ya kuikabidhi kwa kikundi cha wajasiliamali wa mtaa wa ukombozi vingunguti.
Naibu Meya wa Manispaa ya Ilala na Diwani wa Vingunguti, Omary Kumbilamoto akihutubia wakazi wa vingunguti katika mkutano wa hadhara.
Mwanamuziki wa muziki wa Taarabu ,Fatma Mcharuko akitoa burudani katika mkutano huo.
wakazi wa vingunguti wakifatilia mkutano huo.

Vijana Wajasiriamali watakiwa kutokata tamaa

0
0
Vijana wanaojishughulisha na ujasiriamali wametakiwa kutokata tamaa na matatizo mbalimbali wanayokumbana nayo wakati wa shughuli zao.wito huo umetolewa na mfugaji Jonathan Tarimo mkazi wa mkazi wa Migungani kata ya Mto wa Mbu wilaya ya Monduli mkoani Arusha anayejishughulisha na ufugaji 

kijana huyo miezi mitano iliyopita aliwezeshwa kupitia mpango wa Airtel FURSA msimu wa pili kwa kupatiwa ng’ombe wawili, banda la kisasa na mafunzo ya biashara.Akiongea na maofisa wa Airtel waliotembelea katika mradi wake wa ufugaji ili kujionea maendeleo ya biashara yake alisema kwamba amepata matatizo katika shughuli yake baada ya ng'ombe aliyekuwa anampa maziwa kufa.

“nawashukuru sana Airtel kwa kunisaidia kufikisha hapa nilipo sasa, maana nlikuwa na ngo’mbe mmoja tu na Airtel kupitia Airtel Fursa kwa kunipatia ngombe wawili ambapo mmoja alizaa na nikawa nauza maziwa kwa wingi lakini baadae alifariki kutokana na ugonjwa. Kwahiyo nikawa nimebakiwa na ng’ombe wawili na ndama.

Kwa sasa ndama anaendelea vizuri na huyu ngo’mbe mwingine niliyewezeshwa anamimba. Kwasasa changamoto kubwa ni kutafuta chakula kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa nimekuwa nikienda umbali mrefu ili kupata chakula cha mifugo yangu”.

alisema, pamoja na adha aliyoipata, aliwaasa vijana wenzangu tusikate tamaa na kuendelea kutafuta fursa mbalimbali zitazoweza kufikisha katika malengo yao hata kama wakipata changamoto mbalimbali

Naye Afisa masoko Airtel mkoa wa Arusha Geoffrey Sayore alisema, Jonathan amekuwa ni mfano mzuri wa kijana aliyewezeshwa na Airtel FURSA na kuweza kupiga hatua kwenye biashara yake pamoja na changamoto mbalimbali zinazomzunguka.

Nawasihi vijana wanapopata fursa waweze kuzitumia vizuri ili ziwasaidie kuongeza kipato na kutoa ajira kwa jamii inayowazunguka. Lengo letu sisi Airtel ni kuhakikisha vijana wanafaidika na mradi huu wa Airtel Fursa na ndio maaana tunafanya ziara hii kutadhimini mafanikio , changamoto na maeneo ya kuwawezesha zaidi ili kuzifikia ndoto zao na kuwawezesha vijana wengi zaidi.

Airtel FURSA ni mradi wa kijamii kutoka Airtel Tanzania wenye lengo la kuwawezesha vijana wajasiriamali kwa kuwapatia vitendea kazi na elimu ya ujasiriamali ili kuboresha biashara zao.

Afisa masoko Airtel mkoa wa Arusha Geoffrey Sayore (kushoto) akipata maelezo juu ya faida za ng’ombe aliyewezeshwa kijana mjasiriamali anayejishughulisha na ufugaji Jonathan Tarimo (kulia) na Airtel kupitia mpango wake wa Airtel FURSA “Tunakuwezesha” baada ya kumtembelea katika Kijiji cha Migungani ‘B’ wilayani Monduli mkoa wa Arusha na kujionea maendeleo yake pamoja kupanga jinsi yakuboresha zaidi biashara yake.
Jonathan Tarimo (kushoto) kijana mjasiriamali anayejishughulisha na ufugaji akimwonyesha Afisa masoko Airtel mkoa wa Arusha Geoffrey Sayore (kulia) ndama wa mmoja wa ng’ombe aliyewezeshwa na Airtel kupitia mpango wake wa Airtel FURSA wakati Airtel ilipomtembelea ili kujionea maendeleo yake katika Kijiji cha Migungani ‘B’ wilayani Monduli mkoa wa Arusha.

TTCL yadhamini michuano ya vyuo Soka la Ufukweni

0
0
Mkuu wa Biashara Kanda ya Dar es salaam wa Kampuni ya Simu nchini Tanzania (TTCL), Jane Mwakalebela (wa tatu kushoto) akimkabidhi nahodha wa timu ya Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es Salaam (CBE), Ally Rabi (wa tatu kulia) fedha shs 600,000/- pamoja na laini za TTCL za 4G LTE zenye muda wa maongezi wa simu na intaneti (10GB) kwa muda wa mwezi mmoja baada ya kuibuka washindi wa Mashindano ya Mpira wa Miguu wa Ufukweni 'TTCL Inter College Beach Soccer'. CBE ilikifunga Chuo cha Ardhi mabao 2-0 katika mchezo wa fainali uliofanyika Ufukwe wa Coco Beach jijini Dar es Salaam.

Wachezaji wa timu ya Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es Salaam (CBE), wakiwa katika picha ya kumbukumbu na Mkuu wa Biashara Kanda ya Dar es salaam wa Kampuni ya Simu nchini Tanzania (TTCL), Jane Mwakalebela (wa nne kushoto) mara baada ya kukabidhiwa zawadi ya fedha shs 600,000/- pamoja na laini za TTCL za 4G LTE zenye muda wa maongezi wa simu na intaneti (10GB) kwa muda wa mwezi mmoja baada ya kuibuka washindi wa Mashindano ya Mpira wa Miguu wa Ufukweni 'TTCL Inter College Beach Soccer'. CBE ilikifunga Chuo cha Ardhi mabao 2-0 katika mchezo wa fainali uliofanyika Ufukwe wa Coco Beach jijini Dar es Salaam. 


Mapambano mbalimbali ya mechi za Mashindano ya Soka la Ufukweni 'TTCL Inter College Beach Soccer' yakiendelea. 


VITUKO USWAHILINI: AVAA DERA LA MKEWE BAADA YA KUPIGIWA SIMU YA HELA!

0
0
Uswahilini ni sehemu ambayo inaongoza kwa vituko, ugomvi na maneno ya shombo. Wahenga  walisema kuishi kwingi ndio kuona mengi,  Haraka Haraka haina baraka  hii misemo inamaanaisha ukiishi sehemu tofauti tofauti utaona vitu vingi na kujifunza pia. Haraka haraka haina baraka hii imebeba maana ya kwamba ukienda haraka unaweza kukosea au kusahau kitu muhimu.


Tumia dakika zako chache kuitazma short video, ya uswahilini iliyo chezwa na Vicent Petro (Mr.Kilaka) Husina, Moses & Ziada Mgwassa (Zaydar). Endelea kusapport sanaa ya Tanzania tunaamini bila wewe hatuwezi fika popote thanks. Kwa maelezo na taarifa yeyote wasiliana nasi kwenye 0658161950.

BEI YA MADAFU YA LEO

NAMNA BORA YA KUEPUKA HASARA UNAPONUNUA ARDHI.

0
0

Na  Bashir  Yakub.


Wakati  mwingine  ununuzi  wa  ardhi   huweza  kuchukua  muda. Hii  ni  kutokana  na  mazingira ya ardhi  yenyewe  inayouzwa  au  kununuliwa  inavyokuwa.  Wakati  ununuzi  unachukua  muda  pia  huweza   kuchukua  gharama.  Gharama  hizi  zaweza  kuwa  zinatolewa na  mtu    anayetaka  kununua  au  anayetaka  kuuza.


Ifahamike  mapema kuwa  ardhi  hapa  tunazungumzia  viwanja, nyumba na  majengo.

Swali  letu  litakuwa ni je gharama  hizi  zinalindwaje na  sheria  ili  mtu  asiingize  gharama  halafu   kuuziwa  akauziwa  mtu  mwingine. Kabla  ya  hilo hapa  chini tuzijue  gharama  zinazoweza  kuingizwa  kabla  ya  kununua. 


1.  GHARAMA   KABLA  YA KUNUNUA  ARDHI.

( i )   Mnunuzi  katika  kutaka  kujiridhisha   kama  muuzaji  kweli  ni  mmliki   halali na  ikiwa ardhi  haina  mgogoro  hutakiwa  kufanya  upekuzi  maalum( official search).  Upekuzi  huu  hufanyika  ardhi  na  huwa  ni gharama . Ada  lazima  ilipwe  kabla  ya  upekuzi.


( ii )   Gharama  za  mwanasheria. Kwasababu  ununuzi  ni  mchakato  wa  kisheria  basi wanunuzi  huwaingiza  wanasheria katika  mchakato  huu   tangu  anapoiona  ardhi, kuipenda  na  kutangaza  kuinunua  kutoka  kwa  mmiliki. Kwasababu  mwanasheria  atampa  ushauri  wa  awali,  atamwandalia  maombi  ya  upekuzi,  atamsaidia  kukagua  hati  miliki na  mengine mengi, basi  gharama  za  awali  kabla  ya  mkataba  wa  ununuzi lazima  hutolewa.


( iii )  Wengine huwasaidia  wauzaji   katika  gharama  za mchakato  wa  kuteuliwa  kusimamia  mirathi  ili  waweze  kuwauzia ,  na  wengine  huwasaidia  wauzaji  kuwalipia  madeni  ili  ardhi  iwe  huru  na  iweze  kununulika.  


( iv )  Gharama  nyingine  huhusisha  upekuzi ( official  search)  BRELA  iwapo  mchakato  unahusisha  kampuni  mbili  au  hata  moja.  Hutakiwa  kulipia  ada  BRELA  ili  waweze  kukupatia  taarifa  za uhai,  ufu,   au  hadhi  ya  kampuni  kwa  muda  huo.


Gharama zote hizi  na  nyingine  nyingi  hutolewa  na mnunuzi  mtarajiwa  kwa  kutegemea ahadi   aliyopewa  na  muuzaji   kuwa  atamuuzia  yeye  na  si  vinginevyo.


2.  HATARI (RISKS)  YA  KUTOA  GHARAMA   KABLA.

Unaweza  kuwa  umetoa  gharama  hizi  ukiamini  kabisa   kuwa  baada  ya  kila  kitu  kwenda  vizuri   wewe  ndiye  utakayeuziwa  hiyo  ardhi.  Badala yake   muuzaji  akapata   mtu  mwingine  mwenye   ofa  kubwa   akakukwepa  na  kumuuzia  huyo  mtu.


Wakati  huu  hatajali  gharama  ulizokwisha  ingiza  katika  mchakato  wala  muda mwingi  uliopoteza  katika  kufuatilia  mchakato.  Ni  katika  mazingira haya   ambapo  mnunuzi  hutakiwa  kulindwa  na  mkataba  maalum  kabla  hajanunua  ardhi.



MVUA YAWAATHIRI WANANCHI WILAYANI RUNGWE MKOANI MBEYA

0
0
Dotto Mwaibale, Mbeya

WAKAZI wa Vijiji vya Ndubi, Mpuguso Kata ya Kisondela Tarafa ya Pakati wilayani Rungwe mkoani Mbeya wameathiriwa na mvua kubwa iliyoambatana na upepo ambayo imeezua baadhi ya mapaa ya nyumba na kuangusha migomba.

Akizungumza kuhusu tukio hilo mkazi wa Kijiji cha Ndubi, Ambokile Mwangosi alisema wamepata pigo kubwa kutokana na mvua hiyo iliyonyesha mwishoni mwa wiki kutokana na migomba mingi kuanguka hivyo kutishia tishio la njaa.

"Siwezi kuelezea kwa undani tathmini ya athari ya mvua hii lakini tumepata pigo kwani kaya nyingi migomba imeangushwa na mvua hiyo" alisema Mwangosi.Mkazi mwingine wa kijiji hicho Julius Mwambola alisema mvua hiyo imeangusha migomba yake 100 yenye thamani ya sh.250,000.

"Tumeathiriwa kwa kiasi kikubwa na mvua hii kwani mimi binafsi migomba iliyoangushwa na upepo wa mvua hiyo ni zaidi ya 100" alisema Mwambola.Mkazi mwingine wa Kijiji cha Mpuguso kitongoji cha Nkuju, Tulinagwe Naswila alisema mvua hiyo imeangusha migomba yake 40 yenye thamani ya sh.200,000.

Alisema mvua hiyo ilianza kunyesha saa saba mchana na ilidumu kwa muda wa saa moja na kuleta athari kubwa ya kubomoa baadhi ya nyumba na kuharibu migomba."Mvua ilikuwa kubwa ambayoiliharibu migomba na kuezua paa za nyumba kadhaa na kubomoa nyumba ya mjane mmoja aliyemtaja kwa jina la Gwanaloli Ndapapa (85).

Jitihada za kumpata Mkuu wa Wilaya ya Rungwe, Julius Chalya ili kuzungumzia suala hilo zilishindikana baada ya kupigiwa simu mara kadhaa bila ya kupokelewa.


Mkazi wa Kijiji cha Ndubi kilichopo wilayani Rungwe mkoani Mbeya, Julius Mwambola (kulia), akionyesha migomba iliyoangushwa kutokana na mvua iliyonyesha wilayani humo mwishoni mwa wiki. Kulia kwake ni mke wake Nabwike Swebe.
Migomba ikiwa imeanguka kutokana na mvua hizo.

Mwanahabari Dotto Mwaibale, akichukua taarifa ya athari ya mvua hiyo kutoka kwa mkazi wa Kijiji cha Ndubi, Ambokile Mwangosi.

Nyumba ya Kikongwe, Gwanaloli Ndapapa ikiwa imeezuliwa paa na mvua hiyo ya upepo.
Kikongwe Maria Kamendu (85), akiwa ameshika paa la nyumba ya jirani yake Gwanaloli Ndapapa iliyobomolewa na mvua iliyonyesha mwishoni mwa wiki katika Kijiji cha Ndubi wilayani Rungwe mkoani Mbeya na kuharibu migomba na baadhi ya nyumba.

SIMBA NA YANGA KESHO NI MECHI YA KISASI, KUFA NA KUPONA

0
0
Uwanja wa Amaan,  Zanzibar
Na Humphrey Shao, 
Globu ya Jamii 
Ikiwa ni miezi kadhaa tangu watani wa jadi, Simba na Yanga wakutane katika mchezo wa ligi kuu ya Vodacom huku wakitoka suluhu ya bao 1 kwa 1 na kuacha wapenzi wa soka nchi nzima wakiwa na kiu ya kuona mmoja wa timu hiyo inamfunga mwenzake ili wataniane vizuri. 
Mara baada ya mchezo huo kila shabiki alikuwa akizungumza kuwa aina mbaya tutakutana mzunguko wa pili tutakutana mzunguko wa pili na huku wengine wakisema mna bahati hakuna mtani jembe. 
Ikiwa zimebakia saa kadhaa kama sio siku moja kwa timu hizi zinaptaraji kushuka dimbani katika mchezo wa nusu fainali wa kombe la Mapinduzi visiwani Zanzibar hali imekuwa kimya kwa mashabiki wa soka  kusubiria mtanange huo wa aina yake. 
Nathubutu kusema hii ni mechi ya kisasi ambayo ilikuwa ikisubiliwa kwa hamu na mashabiki wa soka hili iweze kuamua nani mbabe kwa miaka hii miwili ya soka . Hivyo kimeeleweka sasa ni Simba na yanga tena uwanja wa Amaan Zanzibar. Jumanne saa 2:15 usiku. 
Hii ni mechi ya tano kwa watani wa jadi kwenye uwanja huo. Mechi 2 fainali ya kombe la Kagame ambapo mwaka 1975 Yanga ilishinda 2-0, mwaka  1992 Simba ilishinda kwa penalti baada ya kutoka sare 1-1 . Simba ilishinda mechi ya ligi kuu 1-0 na fainali ya kombe la mapinduzi 2-0. 
Mechi hizo nne zinaonyesha Simba ikiwa na Historia ya kuifunga Yanga mara nyingi katika Uwanaja wa Amani. 
Hivyo basi tusubiri mchezo huo utakavyopigwa je Simba Historia itambeba au Yanga ndio itakuwa inafuta uteja ndani ya uwanj huu wa Amani.

WANAWAKE MKO WAPI UCHAGUZI MDOGO?

0
0

 Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.


Hivi karibuni Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilitangaza kufanya uchaguzi mdogo wa Ubunge pamoja na Udiwani kwa sehemu mbalimbali nchini ambazo viongozi wake wamefariki au wamepoteza sifa za kuendelea kuongoza wananchi katika sehemu husika.

Uchaguzi huo unategemewa kufanyika Januari 22 mwaka 2017 katika Jimbo la Dimani lililopo Zanzibar pamoja na Kata 20 ambazo zipo kwenye Halmashauri 19 za Tanzania Bara.

Mnamo Desemba 2016, NEC ilifanya uteuzi wa wagombea watakaogombea katika uchaguzi huo ambapo walioteuliwa kugombea Ubunge katika Jimbo la Dimani ni 11 ambao wote ni wanaume na kwa upande wa wagombea udiwani katika Kata mbalimbali za Tanzania Bara ni 71 ambapo wanaume ni 67 na wanawake ni watano.

Kwa kuangalia takwimu hizi chache tu zinatosha kutupatia majibu kuwa katika uchaguzi huu wanawake hawajajitokeza kabisa kugombea nafasi hizo wakati asilimia kubwa ya wanawake nchini wana sifa za kugombea nafasi hizo. Kwa uchaguzi huu wanawake wamewaangusha Watanzania wengi ambao wana amini kuwa wanawake wakipewa nafasi wanaweza kuzitendea haki.

Kumekuwa na wadau wengi duniani wanaotetea haki za wanawake kila kukicha kuhakikisha wanawake wanakuwa na haki sawa na wanaume kwenye nyanja mbalimbali zikiwemo za uongozi, kazi pamoja na elimu.

Pamoja na utetezi huo kushika kasi hadi kufanya jamii nzima kuamini kuwa wanawake wanaweza lakini bado wanawake wengi wanajirudisha nyuma kwa kutojiamini kama wanaweza kushika nyazfa mbalimbali za uongozi nchini.

KUSOMA ZAIDI BOFYA HAPA

WATAKAOZIDISHA NAULI ABIRI KUKIONA-SUMATRA TANGA.

0
0

MAMLAKA ya Usimamizi wa vyombo vya usafiri wa nchi kavu na Majini (Sumatra) mkoani Tanga kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Kitengo cha Usalama Barabarani wameanza operesheni maalumu kwa madereva wanaozidisha abiria na nauli kwenye mabasi yanayotoka  mikoa mbalimbali ikiwemo kanda ya kaskazini.

Hatua inafuatia idadi kubwa ya abiria ambao wanatoka mikoa hiyo kurejea mkoani Tanga na maeneo mengine hivyo baadhi ya mabasi wanapandisha nauli kiholea na kuzidisha abiria.

Hayo yalisemwa na Ofisa Sumatra Mkoani Tanga, Dkt Walukani
Luhamba (Pichani Juu) wakati akizungumza na mtandao huo ambapo alisema waliamua operesheni hiyo ili kuweza kudhibiti masuala hayo ambayo yamekuwa yakiwapa wakati mgumu wananchi wanaotumia vyombo hivyo kwa ajili ya matumizi yao.

Operesheni hiyo inafanyika kwenye maeneo ya Mombo,Korogwe, Mkata na Segera ikiwa ni mkakati wa kuhakikisha wanakabiliana na hali hiyo ili kuweza kuikomesha kwa madereva wenye tabia kama hiyo.

Dkt Walukani alisema katika kuhakikisha wanazibiti operesheni hiyo hivi sasa wanamshikilia dereva wa basi la Hood Issa Kayela (30) linalofanya safari zake kutoka mkoani Arusha kuelekea Mbeya anashikiliwa na Jeshi la Polisi katika kituo cha Mkata wilayani Handeni mkoani Tanga kwa kosa la kuzidisha abiria zaidi ya idadi aliyotakiwa kubeba.

Alilitaja basi hilo lilikuwa na namba za usajili T.779 AVL Scania aina ya Torino lilikuwa likitokea mkoani Arusha kuelekea Mbeya ambapo baada ya kumkamata walimpelekwa mahakamani na baada ya kufika huko akukosa dhamana amerudishwa mahabusu na baade ya wiki mbili anatarajiwa kupandishwa kizimbani.

KUSOMA ZAIDI BOFYA HAPA

SERIKALI YATAKIWA KUJIPANGA KATIKA UJIO WA VIWANDA –TPSF

0
0
Na Chalila Kibuda, Globu ya Jamii

MFUKO wa Sekta Binafsi nchini (TPSF) umesema ujio wa viwanda 200 kutoka nchini China,Serikali inatakiwa kujipanga kupokea viwanda hivyo kwani vitachangia kukua kwa uchumi pamoja na ajira nchini.
 
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF, Godfrey Simbeye amesema China kwa sasa ni nchi yenye mitaji mikubwa kuliko nyingine duniani hivyo lazima kuongeza mahusiano zaidi ili kuweza kunemeeka  nao katika kuelekea uchumi wa kati wa viwanda kufikia 2025.
 
Simbeye amesema viwanda vingi vya China vimefikia hatua ya kuweza kuhamishwa katika sehemu mbalimbali katika Bara la Afrika na kuendelea na uzalishaji kutokana na uhakika wa rasilimali watu pamoja na malighafi.

Amesema  kutokana na uwekezaji wa viwanda hivyo suala la maeneo tengefu  liangaliwe kimkakati   katika kufanya maandalizi  ya viwanda hivyo pamoja na vingine vitakavyojengwa.Simbeye amesema nchi ya China ina uwezo mkubwa wa mitaji kuliko maeneo mengine duniani na Tanzania inaelekea katika uchumi wa viwanda  zilizowawezesha  kufanya mapinduzi ya viwanda.
 
Aidha amesema ujio wa Waziri wa Mambo ya Nchi wa China nchini  ni sehemu ya kuchangamkia fursa kwa karibu kwa kuongeza uhusiano uzidi kudumu ambao wenye maendeleo baina ya nchi mbili.
 
.Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Sekta Binafsi Nchini (TPSF), Godfrey Simbeye akizungumza na waandishi habari juu ujio wa viwanda 200 vya China kuhamishiwa Nchini iliyofanyika jijini Dar es Salaam. 
 Mkuu wa Kitengo cha Masuala ya Uwekezaji na  Maendeleo  ya Biashara wa TPSF, Edward Furaha akizungumza na waandishi habari juu ujio wa viwanda iliyofanyika  jijini Dar es Salaam, Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF, Godfrey Simbeye.
 

MWAKYEMBE ATEMBELEA MAHAKAMA MAALUM YA RUSHWA NA UHUJUMU UCHUMI

0
0
Waziri wa mambo ya katiba na Sheria Dkt Harrison Mwakyembe ametembelea Divisheni Maalum ya Mahakama inayojishughulisha na makosa ya rushwa na uhujumu uchumi nchini Kanda ya Dar es Salaam na kujionea namna inavyoendesha shughuli zake.

Akizungumza katika ziara hiyo Waziri Dkt Mwakyembe amewataka watendaji wa mahakama hiyo kuzingatia lengo la uanzishwaji wa mahakama hiyo ili kuleta tija na ufanisi uliofanywa kuanzishwa kwake.

“Mahakama hii ni chombo maalum kilichoundwa ili kushughulikia masuala ya rushwa na uhujumu uchumi ndani ya muda mfupi, nyinyi kama watendaji hamna budi kuongeza bidii na kuhakikisha mashauri yote yanayoletwa katika mahakama hii yanamalizika ndani ya muda mfupi huku mkizingatia haki za kila mmoja na hivyo kufanikisha lengo la kuanzishwa kwake ”,alisema Dkt Mwakyembe

Aidha alisema uanzishwaji wa mahakama hiyo ulilenga kuifanya Tanzania kupunguza utendaji wa makosa ya aina hiyo au kuyamaliza kabisa na kuongeza kuwa kwa hali ilivyo sasa inaonekana kuwa uhalifu wa aina hiyo umepungua.

Kutokana na kupungua kwa makosa hayo mhe. Waziri alisema anafikiria kuandaa mpango wa kupunguza kiwango cha gharama za makosa ambayo yatapelekwa mbele ya mahakama hiyo . “Inaonekana yale makosa ya ufisadi mkubwa hakuna kwa sasa na hili no moja ya lengo la kunazisha mahakama hii na kwa hali hiyo nafikiria kuja na mpango wa kupunguza kiwango cha thamani ya makosa ambayo kitakuwa ni chini ya kile kilichowekwa awali cha sh. Bilioni moja,” alisema Dr. Mwakyembe.
 Waziri wa Mambo ya Katiba na Sheria Dkt Harrison Mwakyembe akiangalia chumba cha kuendeshea kesi katika mahakama ya makosa ya rushwa na uhujumi uchumi alipoitembelea leo
 Waziri wa Mambo ya Katiba na Sheria Dkt Harrison Mwakyembe akiangalia chumba cha kuendeshea kesi katika mahakama ya makosa ya rushwa na uhujumi uchumi alipoitembelea leo
  Waziri wa Mambo ya Katiba na Sheria Dkt Harrison Mwakyembe akimsikiliza kaimu mkuu wa mahakama hiyo Kanda ya Dar es Salaam Mhe. Jaji Winnie Koroso alipokuwa akiatoa taarifa ya utendaji wa mahakama hiyo  alipoitembelea leo
 Waziri wa Mambo ya Katiba na Sheria Dkt Harrison Mwakyembe akizungumza baada ya kufanya ziara katika Mahakama malum ya makosa ya Rushwa na Uhujumu uchumi Kanda ya Dar es Salaam leo
Waziri wa Mambo ya Katiba na Sheria Dkt Harrison Mwakyembe akiangalia kitabu ambacho huingizwa orodha ya mashauri yaliyofunguliwa katika Mahakama maalum ya makosa ya rushwa na ufisadi alipoitembelea leo.

HABARI ZAIDI BOFYA HAPA

WAZIRI MKUU MAJALIWA AKUTANA NA WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA CHINA OFISINI KWAKE JIJINI DAR

0
0
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Tanzania itaendeleza ushirikiano na Serikali ya China katika nyanja mbalimbali kupitia uwekezaji kwenye sekta ya viwanda, nishati na miundombinu.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumatatu, Januari 9, 2017) alipokutana na Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Mheshimiwa Wang Yi, kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Dk. John Magufuli kwenye makazi ya Waziri Mkuu, Oysterbay jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu amesema ushirikiano wa Tanzania na China ni wa kihistoria, hivyo ameihakikishia Serikali ya China kwamba utaendelezwa kwa manufaa ya wananchi wa Mataifa yote mawili.Aidha, Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji kutoka nchini China kuja kuwekeza katika sekta mbalimbali nchini zikiwemo za miundombinu, viwanda, kilimo na nishati.

“Tanzania iko tayari kupokea kampuni zaidi za China kuja kuwekeza katika maeneo mbalimbali nchini.Tupo tayari kupokea viwanda kati ya 200 hadi 700 katika kipindi cha miaka mitatu ijayo,” amesema.

Kwa upande wake Mheshimiwa Wang Yi amepongeza utendaji kazi wa Mheshimiwa Rais Dk. Magufuli pamoja na viongozi wengine hususan katika mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi na tayari matunda yameanza kuoneka.“Serikali ya China kwa sasa iko katitka mkakati wa kuhamishia viwanda vyake vingi Barani Afrika. Iliamua kuichagua Tanzania kuwa moja katika ya nchi watakayohamishia viwanda hivyo kutokana na kuridhishwa na dhamira inayoonyeshwa na Serikali katika kuleta maendeleo,” amesema.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S. L. P. 3021,
JUMATATU, JANUARI 9, 2017

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China, Wang Yi (kulia kwake) kwenye makazi yake, Oysterbay jijini Dar es salaam Januri 19, 2017. Kushoto kwake ni Waziri wa mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Augustine Mahiga na wanne kulia ni Balozi wa China nchini, Lu Youqing. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu Mhe.Kassim Majaliwa akimkaribisha Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Wang Yi ofisi Ofisini kwake Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya Mazungumzo mafupi. Waziri Wang Yi yupo nchini kwa ziara ya siku moja.

UZINDUZI WA MRADI WA UJENZI WA MIUNDOMBINU MAENEO HURU YA UCHUMI FUMBA.

0
0
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein na Mwenyekiti wa Kampuni ya Azam Group Bw.Said Salim Bakhresa wakifungua pazia kama ishara ya Uzinduzi wa Mradi wa Ujenzi wa Miundombinu katika maeneo huru ya Uchumi huko Fumba Wilaya ya Magharibi "A" Mkoa Mjini Magharibi leo, sambamba na uwekaji wa jiwe la msingi nyumba za kuishi katika shamra shamra za maadhimisho ya miaka 53 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar(Picha na Ikulu)

RAIS MAGUFULI KUFANYA ZIARA MKOANI SIMIYU

0
0

Na Stella Kalinga, Simiyu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli anatarajia kufanya ziara ya siku mbili Mkoani  Simiyu, kuanzia tarehe 11/01/2017 hadi tarehe 12/01/2017.



Akizungumza na Waandishi wa Habari ofisini kwake leo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka amesema, Tarehe 11/01/2017 Rais Magufuli ataweka jiwe la Msingi katika Hospitali ya Mkoa wa Simiyu katika Mtaa wa Nyaumata Halmashauri ya Mji wa Bariadi na kufungua barabara ya Lamadi-Bariadi.



Mtaka amesema baada ya kuweka jiwe la msingi la Hospitali ya Mkoa na kufungua barabara ya Lamadi–Bariadi Mhe. Rais atazungumza na  wananchi wa Bariadi katika Uwanja wa Shule ya Msingi Somanda, mahali lilipo jiwe la ufunguzi wa barabara hiyo.



Aidha, Mtaka ameongeza kuwa Siku ya tarehe 12/01/2017 Mhe.Rais atatembelea kiwanda cha kutengeneza Chaki kilichopo Wilayani Maswa na baadaye ataweka jiwe la msingi katika barabara ya Mwigumbi-Maswa ambapo pia atazungumza na wananchi wa Wilaya ya Maswa.



“Kwa niaba ya Viongozi wa Mkoa wa Simiyu,napenda kuwaalika wananchi wote wa mkoa wetu kujitokeza kwa wingi kumlaki na kumsikiliza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli katika maeneo yote atakayopita”  amesema Mtaka.

 Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na waandishi wa habari(hawapo pichani) katika mkutano aliotisha kwa lengo la kuwajulisha ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli mkoani Simiyu.
Baadhi ya waandishi wa habari wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtakakatika Mkutano aliotisha kwa lengo la kuwajulisha ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli mkoani Simiyu.
Viewing all 109593 articles
Browse latest View live




Latest Images