Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.
BENCHI la Ufundi la Kikosi cha Yanga limeweka wazi kuwa hali ya beki wake wa kushoto Oscar Joshua aliyeumia katika mchezo wa kwanza wa kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Mo Bejaia anaendelea vizuri na atarejea uwanjani tena Jumanne kukipiga na TP Mazembe huku beki wa kulia Juma Abdul anaendelea vizuri na anatarajiwa kuanza mazoezi mepesi mepesi.
Abdul alikosa mechi ya awali baada ya kuwa majeruhi kwa kuumia sehemu ya kifundo cha mguu na kuukosa mchezo wa kwanza na nafasi yake ikichukuliwa na Mbuyi Twite. Hata hivyo kwa sasa anaendelea vizuri na daktari ameweka wazi kuwa anaweza kuanza mazoezi na timu itakaporejea ataungana na wenzake.
Mkuu wa Kitengo cha habari na Mawasiliano Jerry Muro (Pichani)amesema kuwa Joshua anaendelwa vizuri na watakaoukosa mchezo huo ni Beki wa kushoto Mwinyi Haji aliyepata kadi nyekundu pamoja na mshambuliaji Amisi Tambwe mwenye kadi mbili za njano alizozipata kwenye mchezo wa marudiano na Segrada Esperanca ya Angola na wa hatua ya makundi na Mo Bejaia.
"Ni wachezaji wawili tu ndiyo watakaokosa mchezo dhidi ya TP Mazembe ambao ni Mwinyi anayetumikia kadi nyekundu na Tambwe mwenye kadi mbili za njano, kwahiyo katika mchezo huo Oscar atarejea tena uwanjani na Abdul anaendelea vizuri ameanza mazoezi mepesi mepesi na pindi timu itakaporejea ataungana nao,"amesema Muro.
Kwa sasa Yanga inaendelea na mazoezi katika jiji la Antalya nchini Uturuki ikiwa inajiandaa na mchezo dhidi ya TP Mazembe ambao utapigigwa Siku ya Jumanne Juni 28 na unatarajiwa kuwa wa ushindani wa hali ya juu hasa baada ya Yanga kupoteza mchezo wao wa awali na wakihitaji matokeo na TP Mazembe wakitaka ushindi ili kujihakikishia nafasi nzuri ya kuingia nusu fainali.