Na Zainab Nyamka
AFISA ushirika wa manispaa ya Temeke, Martin Mwela amezindua mfuko wa akiba na mikopo unaotambulika kama KIUMA wenye lengo la kuinua wanachama katika kuwapatia mikopo ya riba nafuu huku akiwataka wanachama kuwa waaminifu kwenye urejeshaji wa mikopo.
Akizindua ushirika huo kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Temeke, Bi Sophia Mjema, Mwela amesema kuwa ushirika huo unatikiwa kujiendeleza na kuwa na mshikamano kwani siku zote adui wa ushirika wowote ni mwanachama mwenyewe pale anaposhindwa kufanya marejesho kwa wakati na kufanya mfuko kukosa fedha za kujiendesha ikiwemo kuwapatia mikopo wanachama wengine.
"Wanachama ndio mchawi mkubwa wa kufa kwa vyama kadhaa vya ushirika kutokana na kutokupeleka marejesho kwa wakati pamoja na kukifanya kushindwa kujiendesha ukiwemo wanachama wengine kutokupata mikopo kwa wakati,"amesema Mwela. Huku akiwataka kutokujiingiza kwenye mikopo ya Mifuko ya hifadhi ya jamii kama vile NSSF, LAPF na PPF kwani inakuwa na riba kubwa sana ambapo watakuwa watumwa.
Naye Mwenyekiti wa Mfuko huo wa Ushirika, Ally Pilimo amesema kuwa malengo yao ni kuja kufikia benki kwani wameanzia kikundi cha watu 10 na kwa sasa wapo zaidi ya 30 na tayari wameshatoa mikopo kwa robo ya wanachama wa kikundi hicho.
"Ushirika wetu umekua kutoka kikundi cha watu 10 na kwa sasa tupo zaidi ya 30 na tumeshaweza kutoa mikopo kwa robo ya wanachama na wameweza kujiendeleza kiuchumi ikiwemo kufanya biashara mbalimbali,"amesema Pilimo.
Baada ya uzinduzi huo Wanachama wa chama cha ushirika KIUMA wamekabidhiwa vitabu vyao ambavyo watavitumia kwa ajili ya kuweka akiba zao.
Afisa ushirika Manispaa ya Temeke, Martin Mwela akitoa nasaha kwa wanachama wa Ushirika wa KIUMA wakati wa uzinduzi huo katika viwanja vya Mwembe Yanga leo.
Afisa Ushirika Manispaa ya Temeke, Martin Mwela akikabidhi katiba na Cheti kwa katibu mkuu wa Ushirika wa KIUMA,Peter Daud wakati wa hafla ya uzinduzi wa ushirika huo.
Wanachama ya ushirika wa KIUMA wakiwa katika picha ya pamoja na Afisa Ushirika Manispaa ya Temeke Martin Mwela katika uzinduzi wa Ushirika huo leo.