Na Daniel Mbega
TANGU mwaka 1965 ilipoanza Ligi ya soka ya Taifa Tanzania, ubingwa umekuwa wa timu za Dar es Salaam kutokana na timu za mkoa huo kuutwaa kila mwaka. Hii ni kutokana na uwezo wa kimchezo wa timu hizo, hususan Simba na Yanga.
Lakini ubingwa wa Muungano, ligi ambayo ilianzishwa rasmi mwaka 1982 ikizihusisha timu mbili zilizoshiriki Ligi ya Bara na mbili kutoka Ligi ya Zanzibar, umewahi kutwaliwa na klabu za nje ya mkoa wa Dar es Salaam mara tisa katika miaka ya 1984, 1985, 1986, 1988, 1989, 1990, 1992, 1998 na 1999, wakati ule wa Tanzania Bara umetwaliwa nje ya Dar es Salaam mara tano katika miaka ya 1975, 1986, 1988, 1999 na 2000 tangu ligi hiyo ianze mwaka 1965.
Mseto FC ndiyo ilikuwa timu ya kwanza kuupeleka ubingwa wa taifa nje ya Dar es Salaam mwaka 1975 ikifuatiwa na Tukuyu Stars mwaka 1986, Coastal Union ya Tanga 1988, na Mtibwa Sugar ya Morogoro 1999 na 2000.
Timu zilizotwaa ubingwa wa Muungano kutoka mikoa mingini ni KMKM ya Zanzibar mwaka 1984, Maji Maji ya Songea mwaka 1985, 1986 na 1998, African Sports ya Tanga 1988, Malindi ya Zanzibar 1989 na 1992, Pamba ya Mwanza 1990, na Prisons ya Mbeya 1999.
Mwaka 1975 Mseto, ambayo ilikuwa bingwa wa mkoa wa Morogoro, iliwashangaza mashabiki wengi wa soka nchini Tanzania ilipofanikiwa kuwa timu ya kwanza kuupeleka ubingwa wa Tanzania mikoani na kuvunja utawala wa timu za Dar es Salaam zilizokuwa zikiumiliki ubingwa huo kwa kuachiana (Sunderland ‘Simba’ 1965, 1966 na 1973, Cosmopolitans 1967, Young Africans ‘Yanga’ 1968, 1969, 1970, 1971, 1972, 1974).
Mashabiki wa soka wa Morogoro waliokuwa kwenye uwanja wa Taifa Jumamosi Agosti 2, 1975 usiku wakati Mseto ilipotwaa ubingwa kwa kuifunga Nyota FC ya Mtwara kwa mabao 3-1 katika mchezo wa fainali ya kuwania kombe hilo lililokuwa likiitwa Karume Cup, waliingia kichaa kwa kushangilia baada ya mechi huku wakiongozwa na Katibu wa TANU wa mkoa wao, A. Lyander.
Katika mechi hiyo Mseto ilijipatia mabao mawili kupitia kwa Shiwa Lyambiko na moja kupitia kwa Omar Hussein, wakati ambao Said Dogoa ndiye aliyefunga bao pekee la Nyota kwa njia ya penati. Mseto iliingia fainali kwa kuitoa Usalama (Polisi) ya Dar es Salaam kwa mikwaju ya penati 5-3.
Kombe la ubingwa lilikabidhiwa kwao na Kamanda wa Vijana wa TANU, Rajabu Diwani. Kwa ushindi huo Mseto ilijipatia nafasi ya kuiwakilishaTanzania katika mashindano ya Klabu Bingwa ya Soka Afrika Mashariki na Kati pamoja na Klabu Bingwa Afrika.
Katika kipindi hicho Mseto ilikuwa na wachezaji wazuri kama Said Gedegela, Charles Boniface Mkwasa, Hamadan, Vincent Mkude, Ramadhan Matola, Aluu Ally, Shiwa Lyambiko, Hassan Shilingi, Omar Hussein, Spencer na Jumanne Hassan ‘Masimenti’ waliocheza fainali. Mwingine alikuwa Miraji Salum ambaye alikuwa na timu ya taifa, Taifa Stars, wakati huo.
Kufuatia mafanikio hayo kwenye ligi ya taifa, Mseto ilijikuta ikiporwa wachezaji wengi wakiwemo Abdallah Hussein aliyekwenda Coastal Union ya Tanga, Jumanne Hassan aliyekwenda Simba, Charles Boniface Mkwasa na Miraji Salum waliokwenda Yanga na Vincent Mkude aliyekwenda Tumbaku pia ya Morogoro.
Hata hivyo, nayo iliwapata wachezaji kadhaa nyota akiwemo golikipa Patrick Nyaga aliyetoka Yanga baada ya kukataa kucheza chini ya kocha Tambwe Leya kufuatia mgogoro mkubwa ulioleta mgawanyiko mwaka 1976.
Baada ya ushindi wao wa mwaka 1975, Mseto ilifanya sherehe kubwa kuanzia Novemba 7 hadi 9 ikishirikisha maonyesho ya muziki wa dansi, taarab, mauled na mechi za soka ambapo zilialikwa timu mbalimbali zikiwemo Simba na Cosmopolitans kutoka Dar es Salaam.
Yanga, ambayo ndiyo ilikuwa imevuliwa ubingwa mwaka huo, haikualikwa.
Enzi hizo Mseto ilikuwa chini ya kocha Mohammed Hussein Hassan ‘Msomali’ na baadaye ikaongezewa nguvu na kocha wa timu ya taifa, Taifa Stars, Bernard ‘bernt’ Trauttmann ilipokuwa ikijiandaa kuiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya kimataifa.