Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Inj. Gerson Lwenge amezionya Halmashauri za Wilaya za Njombe na Mbarali kuhakikisha fedha za miradi ya maji zinazotolewa na Serikali, zinasimamiwa vizuri na kutekeleza miradi ya maji na si vinginevyo.
Mhe. Lwenge alisema hayo mwishoni mwa juma katika ziara yake ya Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, alipotembelea Wilaya ya Njombe, mkoani Njombe na Wilaya ya Mbarali, mkoani Mbeya katika ziara yake ya kukagua utekelezaji na maendeleo ya miradi ya maji na upatikanaji wa huduma hiyo.
“Naagiza Halmashauri za Wilaya zihakikishe fedha zilizotengwa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji, zisimamiwe vizuri na zitumike kufanya hivyo na zisitumike kwa miradi mingine. Mhe. Rais Magufuli ameazimia kutatua kero ya maji nchini na hatatutakuwa na sababu yoyote ya kutotimiza lengo hilo, na ifikikapo mwaka 2020 tuwe tumefikia asilimia 85 vijijini na asilimia 95 mijini katika kutoa huduma ya maji na hili lipo ndani ya uwezo wetu”, alisema Mhe. Lwenge.
Waziri wa Maji na Umwagiliaji alisema ni wajibu wa watendaji wote wa Serikali kuwajibika ipasavyo katika nafasi zao kila moja, kwani Serikali ya Awamu ya Tano ni ya vitendo na si maneno. Huku akiendelea kusisitiza suala la maendeleo ya Sekta ya Maji ni shirikishi kati ya Serikali na wananchi, na si Serikali pekee ili kuhakikisha tatizo la maji linapatiwa ufumbuzi kwa haraka na mafanikio.
Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Dr. Rehema Nchimbi amemuhakikishia Mhe. Lwenge kuwa wataiunga mkono Serikali kwa kuhakikisha wanashirikiana na wananchi kutunza mazingira na vyanzo vya maji, ili rasilimali hiyo iwepo ya kutosha kwa miaka mingi ijayo na maendeleo ya sekta hiyo yawe endelevu. Dr. Nchimbi alisema watafanya jitihada za kumaliza changamoto za shughuli za kibinadamu zinazoendana kinyume na Sera na Sheria za Mazingira na Maji nchini.
Katika ziara yake hiyo Mhe. Lwenge aliweka mawe ya msingi kwenye miradi ya maji wa vijiji cha Peruhanda, Wilaya ya Njombe na Ubampa, Kata ya Ubaruku, Wilaya ya Mbarali, ikiwa ni kati ya miradi 1,800 inayotekelezwa na Serikali kitaifa na kati ya miradi hiyo, 1,200 ikiwa imekamilika.
Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Inj. Gerson Lwenge akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Ubampa, Kata ya Ubaruku, Wilaya ya Mbarali, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Abbas Kandoro (kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Mbarali, Gulamhussein Kifu.
Mradi wa Maji unaohudumia Kijiji cha Peruhanda, Wilaya ya Njombe.
Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Inj. Gerson Lwenge mara baada kuweka jiwe la msingi kwenye mradi wa maji wa Kijiji cha Ubampa, Kata ya Ubaruku, Wilaya ya Mbarali na Mbunge wa Jimbo la Mbarali, Mhe. Haroon Pir Mohamed.
Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Inj. Gerson Lwenge akitakata utepe na kuweka jiwe la msingi kwenye mradi wa maji katika Kijiji cha Peruhanda, Wilaya ya Njombe, pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Saraha Dumba.
Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Inj. Gerson Lwenge akikagua chanzo cha maji cha Nyenga kinachohudumia Mji wa Njombe, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Njombe (NJUWASA), Inj. Daudi Majani.